Wednesday 16 May 2018

YOUNG BOYS YAIBUGIZA QANDACH FC MABAO 6-0 KWENYE KURUGENZI CUP '18



Mashindano ya Kurugenzi CUP ’18 yaliyoandaliwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara, Hudson Kamoga yameendelea kutimua vumbi leo Mei 16 kwenye viwanja vya shule ya msingi Haydom kwa timu ya soka ya Young Boys kuifunga mabao 6-0 timu ya Qandach FC.

Mabao ya Young Boys yalifungwa na Chunga Elia kwenye dakika ya 9 kwa shuti kali ndani ya eneo la hatari na kumshinda mlinda mlango wa timu ya Qandach FC Israel Petro.



Bao la pili la Young FC lilifunga na Enea Sule kwenye dakika ya 24 kwa kichwa baada ya kupokea krosi kali iliyopigwa kiufundi na winga wao Shondo Silvin aliyevaa jezi nambari 5 mgongoni.

Yule yule mfungaji wa bao la kwanza Chunga Elia mnamo dakika ya 30 aliwainua mashabiki wa timu ya Young Boys ambao walijaa kwenye uwanja huo wa shule ya msingi Haydom licha ya mvua kali kuendelea kunyesha kwa kufunga kwa shuti kali la umbali wa mita 25 na kuandika bao la tatu.

Mchezaji kiungo mkabaji Yoram Thomas wa timu ya Young Boys aliipatia timu yake bao la 4 mnamo dakika ya 49 ya kipindi cha pili kwa kufunga baada ya kutokea piga nikupige langoni mwa timu ya Qandach FC.

Bao la 5 la Young Boys lilifungwa na mchezaji wao machachari Elmalek Malley aliyeingia kuchukua nafasi ya Yoram Thomas kwa shuti kali baada ya kupewa pasi safi na mchezaji Zacharia Simon (Dokta) kwenye dakika ya 78 ya mchezo huo.

Chunga Elia alihitimisha karamu ya mabao kwa timu hiyo kwa kufunga bao la kiufundi la sita baada ya kuwachambua walinzi wa timu pinzani na kuachia shuti kali lililomshinda kipa na kuzama kwenye nyavu ndogo ambapo hadi mwisho wa mchezo huo Young Boys waliibuka kidedea kwa mvua ya magoli 6 na Qandach 0.

No comments:

Post a Comment