HABARI ZA KIMATAIFA

3 comments:

  1. Cameroon yavunja kambi ya mafunzo ya Boko Haram

    Jeshi la Cameroon limeeleza kuwa vikosi vyake vimevunja kambi ya mafunzo ya kundi la kitakfiri la Boko Haram lenye makao yake nchini Nigeria huko kaskazini mwa nchi hiyo. Jeshi la Cameroon limesema kuwa limeivunja kambi hiyo iliyokuwa katika wilaya ya Mayo-Danay kaskazini mwa nchi.

    Wiki iliyopita, wanamgambo wa kundi la kitakfiri na kigaidi la Boko Haram waliishambulia kambi moja ya kijeshi nchini Cameroon karibu na mpaka wa Nigeria, mashambulizi ambayo yalijibiwa na vikosi vya Cameroon na kulisababishia hasara kubwa kundi hilo.

    Wanamgambo wa Boko Haram katika miezi ya hivi karibuni wamezidisha hujuma zao za kigaidi kwa kutekeleza mashambulizi katika maeneo ya mipaka kati ya nchi mbili hizo.

    Kundi la kitakfiri la Boko Haram limedai kuhusika na utegaji mabomu na mashambulizi mengi makubwa katika maeneo mbalimbali ya Nigeria tangu kundi hilo lianzishe hujuma zake mwaka 2009, mashambulizi ambayo hadi sasa yameuwa watu zaidi ya elfu kumi.

    ReplyDelete
  2. Uingereza ina raia wengi katika kundi la Daesh

    Takwimu mpya za hivi karibuni zinaonyesha kuwa Waingereza ndio raia wengi walio katika kundi la kigaidi na kitakfiri la Daesh kati ya nchi za Magharibi.

    Takwimu hizo mpya zinaonyesha kuwa, hadi sasa Waingereza wapatao elfu mbili wamejiunga na kundi la kigaidi la Daesh. Serikali ya Uingereza kitambo nyumba ilitangaza kuwa kwa uchache Waingereza 500 wamejiunga na kundi hilo la kigaidi na kitakfiri. Ripoti iliyotolewa mwezi Oktoba mwaka huu na Umoja wa Mataifa ilionyesha kuwa, raia wa nchi za nje wasiopungua elfu 15 wameleekea Syria na Iraq kwa minajili ya kujiunga na Daesh na makundi mengi ya kigaidi.

    Wakati huo huo habari kutoka Kuwait zinasema kuwa watu watatu waliokuwa wakiliunga mkono kundi la kigaidi na kitakfiri la Daesh wamehukumiwa kifungo cha jela nchini humo. Mahakama moja nchini Kuwait imewahukumu kifungo cha kuanzia miaka 4 hadi 10 jela, watu hao waliokuwa na uhusiano na kundi la Daesh.

    Watu hao watatu ambao wawili ni raia wa Misri na mmoja kutoka Jordan wamehukumiwa kwenda jela kwa tuhuma za kusambaza matangazo kwa lengo la kukusanya misaada kwa ajili ya magaidi wa Daesh.

    ReplyDelete
  3. Al Bashir avikosoa vyombo vya habari vya Magharibi

    Rais Omar al Bashir wa Sudan amevituhumu vyombo vya habari vya Magharibi kwa kutoa picha isiyo sahihi kuhusu hali ya mambo ya nchi hiyo. Rais wa Sudan amesema kuwa vyombo vya habari vya Magharibi na hasa Marekani vimekuwa vikitoa picha mbaya na ya uwongo kuhusu hali ya mambo ya Sudan kwa kuzipotosha fikra za waliowengi duniani.

    Akizungumza mjini Khartoum katika mahojiano na gazeti la Washington Post la nchini Marekani, Al Bashir ameongeza kuwa, kuharibiwa taswira ya Sudan katika vyombo vya habari vya Marekani na nchi nyingine za Magharibi kunadhihirisha nafasi haribifu ya vyombo hivyo katika upashaji habari. Rais Omar al Bashir wa Sudan amesema kuwa, Marekani haitekelezi ahadi zake khususan za kuindolea nchi hiyo vikwazo na kwamba siasa za Washington kwa Sudan zinawaathiri raia wa nchi hiyo. Marekani iliiwekea Sudan vikwazo tangu mwaka 1997 na mwaka 2013 Rais Barack Obama wa nchi hiyo aliongeza muda wa vikwazo hivyo kwa mwaka mwingine mmoja.


    ReplyDelete