Tuesday 22 May 2018

WAKULIMA KITETO WAJENGEWA UWEZO WA KUPAMBANA NA VIWAVIJESHI VAMIZI

 Wataalamu wa kilimo kwa kushirikiana na Shirika la Chakula na Kilimo Duniani ( FAO) wamewajengea uwezo wakulima wa wilaya ya Kiteto Mkoani Manyara juu ya namna ya kupambana na viwavijeshi vamizi vinavyoshambulia zao la mahindi.

Sehemu mbalimbali za mkoa wa Manyara wakulima wengi wanalalamikia mazao yao ya mahindi yaliyopo mashambani hivi yameshambuliwa na wadudu hao.

Wataalamu hao waliwasilisha mada tatu juzi wilayani Kiteto ambazo ni  utambuzi, uchunguzi, ufuatiliaji na udhibiti wa wadudu hao viwavijeshi vamizi.

Akiwasilisha mada ya kwanza ambayo ni utambuzi , Ofisa kilimo Sergea Mutahiwa  alielezea namna ya kumtambua kiwavijeshi vamizi, mzunguko wa maisha yake, tabia zake na muonekano wake.

Pia ameeleza kuhusu hali ya viwavi jeshi nchini, ushirikishwaji wadau, usambazaji wa machapisho, ushiriki wa vyombo vya habari na mtazamo wa jamii kuhusu viwavijeshi vamizi .

Alisema mtazamo wa jamii na uelewa mdogo ni tatizo juu ya uelewa kwa viuatilifu vinavyopendekezwa na jinsi ya kutumia dawa za kuangamiza wadudu hao hatari kwa kushambulia mazao.

Alisema wakulima wameendelea  kutumia viatilifu  vingi vya aina mbalimbali  na katika maeneo mengine wakulima hutumia dozi kubwa kutokana na mashambulizi kujirudia .

Mutahiwa alisisitiza kuwa  matumizi  yasiyo sahihi ya viatilifu yanaweza kusababisha  kuua wadudu wasiolengwa  na  kudhuru afya za binadamu, vilevile kusababisha usugu  kwa visumbufu vya mimea.

Alisema viatilifu vinavyoshauriwa na  Taasisi ya Utafiti wa Viuatilifu (TPRI) na serikali kupitia wizara ya kilimo inatarajia kuzichukua ili  kudhibiti kisumbufu hicho.

Ofisa kilimo Grace David alitoa mada ya ukaguzi na ufuatiliaji kwa kufuatilia ukuaji wa mimea shambani, kwamba mimea inatakiwa kufuatiliwa katika ukuaji wake.

Alielekeza namna ya kufanya ukaguzi kuwa ufanyike zigizaga, usifuate mstari  ili kuwakilisha shamba zima  na usichukue zaidi ya dakika 15.

Alisema ukaguzi ni muhimu ili kubaini  uwepo na kiasi cha viwavijeshi vamizi, na kufanya tathmini ya madhara ili kuweza kujua njia sahihi ya kufanya udhibiti.

Pia, aliwaelezea wakulima hao namna ya kutumia mtego maalum wenye harufu kwa ajili ya kukamata viwavijeshi vamizi.

Ayubu  Nchimbi akitoa mada ya tatu ya udhibiti viwavijeshi vamizi alisema udhibiti wa kiwavijeshi vamizi unaanza na utambuzi.

Nchimbi alisema lazima kumtambua kisumbufu, mzunguko wa maisha yake, dalili za mashambulizi na kiasi gani mashambulizi yamefanyika.

Alisema dalili za  mashambulizi ndizo zitakazomuongoza mkulima  kujua kiasi cha mashambulizi na njia atakazotumia ili kudhibiti kisumbufu.

Alisema udhibiti sahihi wa viwavijeshi vamizi  katika ukuaji wa mimea ya mahindi unategemea na muda wa utambuzi wa mashambulizi ya mdudu kupitia ufuatiliaji na ukaguzi wa mimea shambani.


No comments:

Post a Comment