Wednesday 16 May 2018

KURUGENZI CUP '18 YAZINDULIWA NA DED KAMOGA

IMG-20180515-WA0004

Mji mdogo wa Haydom wa Wilayani Mbulu Mkoani Manyara na viunga vyake kwa muda wa wiki hii nzima utakumbwa na burudani kubwa kupitia tamasha la ujasiriamali na michuano ya Kurugenzi Cup '18 iliyoandaliwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya hiyo, Hudson Kamoga. 

Pamoja na mada za ujasiriamali kutolewa pia michuano ya soka itakayoshirikisha timu 10 itatimua vumbi kwenye viwanja vya Haydom. 




Kamoga alisema anatarajia vijana watajinyanyua kiuchumi kwa kufanya kazi kupitia kauli mbiu ya tamasha hilo isemayo wakati wa kuwa mzalendo na kujenga nchi yetu, uvivu ni sumu ya maendeleo. 

Alisema kwa muda wa wiki moja itakayofanyika tamasha hilo kutakuwa na mada mbalimbali za ujasiriamali zitakazotolewa na magwiji mbalimbali waliobobea kwenye uchumi. 




"Wilaya ya Mbulu ina fursa nyingi na vichocheo vya kiuchumi hivyo tutawatumia watu maarufu akiwemo mchambuzi wa soka Shafi Dauda ambaye atakuja hapa Haydom," alisema Kamoga. 

Alisema wanatarajia kuibua vipaji vipya tofauti kwenye soka na riadha ili vijana wafuate nyayo za mwanariadha maarufu wa zamani John Stephen aliyeacha historia kwenye michuano ya dunia. 



Katibu wa chama cha soka cha wilaya ya Mbulu (MDSA) Joseph Nicodemus alitaja timu zitakazoshiriki michuano hiyo ni Dongobesh FC, Young Boys, Airport SC, Qadesh SC, Mlimani City Lambo FC, Stand United, Makurusa SC, Rema 1,000 na Kidarafa FC ya wilaya jirani ya Mkalama Mkoani Singida. 

Nicodemus alisema michuano hiyo itakayofanyika kwa muda wa wiki moja itatumia mtindo wa mtoano na siyo ligi, hivyo timu ikifungwa inatolewa mashindanoni. 

Kwenye ufunguzi wa michuano hiyo, timu ya Dongobesh FC iliifunga timu ya Kidarafa FC ya wilayani Mkalama mkoani Singida mabao 2-1. 



No comments:

Post a Comment