Tuesday 22 May 2018

BARAZA LA MADIWANI SIMANJIRO LAPITISHA KUTOLEWA MILIONI 100 ZA MIKOPO

 Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara, limepitisha kutolewa kwa zaidi ya sh100 milioni kwa ajili ya mikopo ya kuwezesha wanawake na vijana kwa lengo la kuwanyanyua kiuchumi.



Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro Jackson Sipitieck akizungumza kwenye kikao cha Baraza la madiwani kilichofanyika mji mdogo wa Orkesumet, alisema fedha hizo zimetokana na asilimia 10 za mapato ya ndani ya halmashauri hiyo.



Sipitieck alisema baraza la madiwani wa halmashauri hiyo wamekuwa na kawaida ya kupitisha fedha hizo ambazo kwa namna moja au nyingine zitafanikiwa kubadili maisha ya vijana na wanawake wa eneo hilo.



“Tumefanikiwa kugawa fedha hizo kwenye kata mbalimbali za halmashauri ya wilaya yetu ambayo  ina kata 18 na tutaendelea kuzigawa kwa haki kwa vikundi vingine vilivyokidhi masharti na vigezo vya kupatiwa,” alisema Sipitieck.



Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya hiyo Yefred Myenzi alisema hadi hivi sasa fedha hizo sh100 milioni zimetolewa kwa vipindi tofauti na kikao cha baraza hilo kimepitisha fedha nyingine sh32.6 milioni zitakazopatiwa kwenye kata sita.



Myenzi alitaja kata hizo sita za Mirerani, Oljoro namba tano, Shambarai, Komolo, Loiborsiret na Msitu wa Tembo ambapo vimetolewa kwa vikundi 16 vya wanawake na vijana wa Simanjiro.



Alisema halmashauri hiyo itaendelea kutoa fedha hizo pindi itakapokuwa inakusanya makusanyo yake ya ndani hivyo wanawake na vijana wachangamkie fursa hiyo kupitia asilimia 10 za mapato ya ndani.



Diwani wa kata ya Loiborsiret, Ezekiel Lesenga Mardadi amewataka wanawake na vijana wa kata hiyo waliopatiwa mikopo hiyo kuitumia kwa malengo sahihi ili waweze kurejesha kwa wakati.



Mardadi alisema endapo vijana na wanawake hao wataitumia vizuri mikopo hiyo watajinyanyua kwenye biashara zao na watarejesha kwa wakati ili wengine nao waweze kufaidika.



Diwani wa kata ya Shambarai Julius Mamasita alisema vijana na wanawake wa kata yake wana ari kubwa ya kutumia mikopo hiyo kwa lengo la kujinyanyua kiuchumi na wametoa ahadi kuwa watafanikisha hilo.



“Naishukuru halmashauri ya wilaya ya Simanjiro kwa kutupatia mikopo hii nasi wananchi wa kata ya Shambarai tutaweza kutumia mikopo hii ipasavyo na kisha kuirejesha kwa wakati,” alisema Mamasita  



No comments:

Post a Comment