Wednesday 21 September 2016

WAWILI WANUSURIKA KUFA MGODINI


WACHIMBAJI wawili haramu wamenusurika kufariki dunia baada ya kuishia hewa walipoingia kwa wizi kwenye mgodi wa kampuni ya TanzaniteOne ya Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara.

Akizungumza na waandishi wa habari, kamanda wa polisi wa mkoa wa Manyara, kamishna msaidizi (ACP) Francis Massawe alisema wachimbaji hao haramu waliingia kwenye mgodi wa TanzaniteOne uitwao Investa.

Kamanda Massawe alisema tukio hilo lilitokea juzi alasiri kwenye mgodi huo baada ya wachimbaji hao kuingia kwa wizi chini kwa chini mgodini kupitia mitobozano na kufanya kazi kwenye mgodi huo ambao hautumiwi hivi sasa.


Aliwataja wachimbaji hao haramu ambao walinusurika kufariki dunia kwa kukosa hewa mgodini ni Ramadhani Juma na Mohamed Jumanne wote wakazi wa mji mdogo wa Mirerani wilayani Simanjiro.

Alisema wanawashikilia watu hao wawili kwa ajili ya mahojiano kabla ya kuwafikisha mahakamani kujibu tuhuma za kuingia kwa jinai kwenye mgodi ambao hawaumiliki wana hawafanya kazi katika mgodi huo.

Hata hivyo, alitoa onyo kwa watu wote wanaowafadhili wachimbaji hao haramu kuzamia bila halali kwenye mgodi wa kampuni hiyo kwani vitendo hivyo huchangia uhalifu kutokana na kufanya kazi eneo ambalo hawalimiliki.


Ofisa uhusiano wa kampuni ya TanzaniteOne Halfan Hayeshi alisema siku ya tukio hilo watu 10 waliingia kwenye mgodi huo wa Investa ambao haufanyiwi kazi kupitia mtobozano uliopo na kuendelea na shughuli zao bila halali.

Hayeshi alisema baada ya kuishiwa hewa kupitia mashine ya jenereta iliyokuwa inatoa hewa ya chafu ya ukaa, watu hao walitoa taarifa kwa mlinzi wa kampuni hiyo ambaye aliwaambia wasubiri atoe taarifa kwa uongozi ndipo wakatoroka.

“Baada ya kufika eneo la tukio tulitoa taarifa polisi na uongozi wa ofisi ya madini Mirerani ndipo tukaanza zoezi la kuwaokoa watu hao ambao tuliwakuta wawili wakiwa na hali mbaya na hadi sasa wanashikiliwa na polisi,” alisema.   

WAANDISHI WAASWA KUFANYA UTAFIKI HABARI ZA GESI NA MAFUTA


Waandishi wa habari nchini wametakiwa kutumia taaluma yao kwa kufanya
utafiti na kuandika ipasavyo habari za mafuta na gesi ili jamii iweze
kutambua namna itakavyonufaika kupitia rasilimali hizo muhimu.


Mkuu wa wilaya ya Arusha Gabriel Daqarro, aliyasema hayo kwenye
mafunzo kwa waandishi wa habari wa mikoa ya Arusha, Kilimanjaro na
Manyara, yaliyotolewa na shirika la maendeleo ya petrol nchini (TPDC).

Daqarro alisema jamii inapaswa kutambua faida itakazopata kupitia
miradi ya maendeleo ya gesi na mafuta ikiwemo ajira, biashara kwani
mara nyingi wasipopatiwa uelewa hupinga mradi na kusababisha hasara
kwa Taifa.

Alisema suala la bomba la mafuta kutoka Tanga hadi Uganda nalo
linapaswa kuandikwa kwa marefu na mapana ili wananchi watakaopitiwa na
mradi huo waone faida itakayopatikana kiuchumi kwa wao binafsi na
Taifa kwa ujumla.

Alisema hata zile vurugu za mikoa ya kusini bado kiini chake
hakijalikana ila hivi sasa wananchi wameelewa faida ya gesi ikiwemo
watu wa Mtwara ambao hivi karibuni umeme ulivyosumbua nchini wao
walinufaika na gesi,” alisema .




Kwa upande wake, ofisa habari wa shirika la maendeleo ya petroli
nchini (TPDC) Francis Lupokela, akizungumza na waandishi hao alisema
wamekuwa wakitoa mafunzo kwa waandishi wa habari ili kuwajengea uwezo
juu ya mafuta na gesi.

Lupokela alisema waandishi wa habari ndiyo wanaohabarisha jamii
kupitia vyombo vyao na wananchi watatambua namna rasilimali ya mafuta
na gesi itakavyowanufaisha pindi wakielezewa kupitia magazeti, tv,
redia na mitandao.

“Hata zile vurugu za awali kwenye baadhi ya mikoa ya kusini ilitokana
na jamii kutoelewa ila baada ya wao kupatiwa elimu kuwa nao
watanufaika na rasilimali hizo hivi sasa hali imetulia na shughuli
zinaendelea ipasavyo,” alisema.

Mwenyekiti wa chama cha waandishi wa habari wa mkoa wa Arusha (APC)
Claud Gwandu alisema suala la elimu ya mafuta na gesi ni muhimu
kutolewa kwa waandishi wa habari ili waweze kufikisha kwa jamii kwa
undani zaidi.

Gwandu alisema waandishi wa habari wangepaswa kupelekwa maeneo ya nje
ya nchi kupata mafunzo ikiwemo nchi ya Norway ambayo iligundua gesi
mwaka 1960 ili kuona wananchi wa eneo hilo walivyonufaika kupitia
nishati hiyo.

“Nakumbuka gesi asilia ya Songosongo iligundulika nchini mwaka 1974
ila baba wa Taifa akasema iachwe kwanza ili watanzania wapate elimu
kwa ajili ya kufahamu na kunufaika na rasilimali hiyo muhimu kwa nchi
yetu,” alisema.


WALIA NA HUDUMA MBOVU KITUO CHA AFYA MIRERANI


Wagonjwa wanaopata huduma kituo cha afya Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, wameiomba Serikali kuchukua hatua na kuboresha matibabu kwenye kituo hicho kwani hivi sasa huduma nyingi zimedorora.

Wakizungumza kuhusu changamoto hiyo wagonjwa hao walidai kuwa huduma zinazotolewa hivi sasa kwenye kituo hicho ni vipimo, kliniki ya mama na mtoto na vidonge vya kufubaza virusi vya ukimwi (ARV) pekee.

Mmoja kati ya wagonjwa hao John Benarld alisema hivi sasa kituo hicho kina hali mbaya mno kwani hata dawa zimekuwa tatizo, hadi kusababisha wagonjwa kudhani kuwa wauguzi wanauza dawa kwenye maduka yao kumbe sivyo.

“Tunaiomba serikali iingilie kati suala hili kwani ni aibu hata maji ya drip hawana, dawa hakuna hata paracetamol hazipo na pia hivi sasa ni zaidi ya miezi mitatu maji ya bomba yamekatika katika kituo hicho cha afya,” alisema Bernald.

Selemani Mohamed alisema hata upungufu wa watumishi ni tatizo kwani alitumia muda wa saa mbili kukaa kwenye kiti kwa ajili ya kupata huduma ya vipimo kwenye maabara kutokana na kuwepo na mtumishi mmoja pekee.

“Nimetoka kwa daktari muda mrefu na mtoto wangu mdogo anaumwa nimeambiwa niende eneo la maabara akachukuliwe kipimo cha damu lakini bado sijapatiwa huduma huyu dada yupo peke yake,” alisema Mohamed.

Alisema kitengo cha maabara kinapaswa kiwe na wahudumu wawili au watatu kwani kuna wagonjwa wengine wanafika kituoni hapo wakiwa wana hali mbaya ya kuzidiwa ila hivi sasa kuna mtaalamu mmoja anayehudumia watu wengi.
Hata hivyo, mganga mfawidhi wa kituo hicho Dk Raymond Msaki alikiri kuwepo na upungufu wa dawa kwani wagonjwa wengi wamekuwa wanakosa huduma kutokana na upungufu huo, ila uongozi ulishafikisha taarifa sehemu husika.

Dk Msaki pia alikiri kuwepo na tatizo la maji kwenye kituo hicho kwani tangu mwezi Julai maji yaliyounganishwa na mamlaka ya mji mdogo hayapatikani ila wakitaka maji wanaomba kwa jirani yao kulikokuwa na shirika la World vision.

“Upungufu wa watumishi ni kweli kwani sehemu ya maabara hivi sasa kuna dada mmoja yeye ndiye anaandika wagonjwa anawapima na kutoa majibu, wenzake wawili hawapo, mmoja yupo masomoni na mwingine yupo likizo,” alisema.

MWENGE MANYARA

 Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Dk Joel Bendera akimkabidhi zawadi mkimbiza mwenge kitaifa kutoka mkoa humo Lucia Kamafa baada ya mwenge huo kuwasili kijiji cha Gunge Wilayani Simanjiro.
 Mkuu wa Mkoa wa Manyara Dk Joel Bendera akisoma taarifa ya mkoa huo mara baada ya mwenge wa uhuru kufika mkoani humo, ambapo miradi ya thamani ya zaidi ya sh7.7 bilioni ilitembelewa.
 Kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru kitaifa George Mbijima akizungumza na wakazi wa Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara.
  Kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru kitaifa George Mbijima akizindua mradi wa maji kwenye Kijiji cha Gunge Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara.
  Mkimbiza mbio za mwenge wa uhuru kitaifa Nahoda akisalimiana na mkurugenzi wa shirika la Mwedo Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara, baada ya mwenge kuzindua jengo hilo.
 Kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru George Mbijima akisikiliza maelezo ya ofisa ushirika wa Halmashauri ya Wilaya ya Hanang’ Mkoani Manyara, Minde Nanagi wakati akizindua soko na ghala lililotumia sh1 bilioni, (kushoto) ni mkuu wa wilaya hiyo Sara Msafiri na (kulia) ni mkimbiza mwenge kutoka mkoa wa Kaskazini Pemba, Nahoda Makame.
  Mbunge wa jimbo la Mbulu Vijijini Flatey Massay akizungumza mara baada ya kuzinduliwa kwa mradi wa maji kwenye eneo hilo.
  Ukiwa Wilayani Simanjiro mwenge wa uhuru pia ulizindua mradi wa biogesi kwenye shule ya msingi Emboreet.
 Kilo 40 na misokoto nane ya bangi ilichomwa moto na pombe haramu ya gongo ilimwagwa mara baada ya mbio za mwenge wa uhuru kuwasili wilayani Kiteto.