Tuesday 22 May 2018

MARDADI ALIA NA MAJI LOIBORSIRET

Diwani wa Kata ya Loiborsiret Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, Ezekiel Lesenga (Mardadi) ameitaka Halmashauri ya Wilaya hiyo kuwaangalia wananchi wake kwa jicho la huruma ili waweze kupata huduma ya uhakika wa maji kwani wengi wao wanatumia maji kidogo yaliyopo kwa kushirikiana na mifugo.

Mardadi alisema wananchi wa kata yake wanaishi kwenye nyanda kame hivyo halmashauri hiyo ifanye jitihada za kuwezesha upatikanaji wa huduma hiyo ili waondokane na kero ya maji.

Alisema suala la tatizo la maji ni kero ya muda mrefu na yeye kama diwani wa eneo husika ataendelea kulisemea hilo hadi ufumbuzi upatikane kwa wananchi wake wa kata ya Loiborsiret.

"Hali ya wananchi wa eneo hilo kwenye huduma ya maji ni ndogo kwani hivi sasa wanategemea mabwawa yaliyojaa maji kutokana na mvua ndiyo wanatumia wao na mifugo," alisema Mardadi.

Alisema wakati wa kiangazi unapofika maji ya kwenye mabwawa hukauka na kuwapa wakati mgumu binadamu na mifugo kupata huduma ya maji.

Alisema kwenye kata yake ya Loiborsiret suala la maji ni tatizo kubwa kwenye vijiji vyote vya Loiborsiret, Kimotorok na Narakauwo.

Alisema anatarajia halmashauri ya wilaya ya Simanjiro italiangalia suala hilo kwa upana zaidi ili huduma ya maji kwenye eneo hilo iwe ya uhakika tofauti na sasa.

"Wakati wa kiangazi jamii ya eneo hilo hupata wakati mgumu kwani maji yanapatikana kwa shida hivyo kusababisha mifugo kufa na wananchi nao wanateseka," alisema Mardadi.

Hata hivyo, Mwenyekiti wa kamati ya Elimu, Afya na Maji wa baraza la madiwani wa Halmashauri ya wilaya hiyo Sendeu Laizer akizungumza mwishoni mwa wiki iliyopita alisema wamepanga kuchimba kisima kimoja kwenye kata hiyo.


"Kamati yetu kwenye mapendekezo yake iliazimia kuchimbwe kisima kimoja katika kijiji cha Narakauwo kata ya Loiborsiret ili jamii ya eneo hilo na mifugo waweze kupata huduma ya maji," alisema Laizer. 

No comments:

Post a Comment