Thursday 13 October 2016

WANYONGE KULIPIWA MATIBABU YA iCHF HANANG'


Wananchi wanyonge ambao ni kaya masikini wamenufaika baada ya Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Hanang’ Mkoani Manyara, George Bajuta, kujitolea sh1.8 milioni kwa ajili ya kuzilipia kaya masikini 36 za watu 216 wa Kata ya Simbay kwenye mfuko wa afya ya jamii iliyoboreshwa (iCHF).

Bajuta ambaye ni diwani wa kata hiyo aliyasema hayo kwenye uzinduzi wa mfuko wa afya ya jamii ulioboreshwa (iCHF) ulioandaliwa na mfuko wa Taifa wa bima ya afya (NHIF) mkoani humo na kudai kuwa kila kitongoji kitatoa kaya tatu za wanyonge wasiojiweza.

Alisema kata yake ina vitongoji 12 na kila kitongoji kitachagua kaya tatu ambazo ni familia za wanyonge zisizojiweza ili awalipie sh30,000 kila kaya yenye watu sita, baba, mama na watoto wanne, zitakazopata huduma za afya kwa mwaka mzima.

“Mimi sina utajiri mkubwa ila nimeamua kujitolea kidogo nilichonacho kwa kuhakikisha wale ndugu zangu wanyonge wasiokuwa na uwezo kabisa kwenye kila kitongoji nao wapate fursa ya kutibiwa bure kwa mwaka,” alisema Bajuta.


Mkuu wa wilaya hiyo Sarah Msafiri akizungumza wakati akizindua mfuko huo alisema wananchi wa eneo hilo wanapaswa kushiriki ipasavyo kwa kujiunga na (iCHF) kwani hadi mwisho wa mwaka inatakiwa asilimia 50 ya watu wajiunge.

“Hapa kwenye Tarafa ya Simbay kuna zaidi ya wakazi 6,200 hivyo tunapaswa kujiunga kwa wingi ili watu zaidi ya 3,100 ambayo ndiyo nusu ya watu ili kutimiza lengo la serikali la kuhakikisha hadi idadi hiyo inafika,” alisema Msafiri.

Meneja wa mfuko wa Taifa wa bima ya afya (NHIF) mkoani Manyara, Isaya Shekifu alisema kila kaya itakayotoa sh30,000 kwa ajili ya kuchangia mfuko huo nayo serikali kuu huchangia nusu nyingine sh30,000 na kuwa sh60,000.

Shekifu alisema iCHF iliyoboreshwa inajenga mfuko endelevu wa kuchangia kijamii gharama za matibabu na kuboresha ubora wa huduma za afya kupitia mafunzo kwa watoa huduma, utoaji vifaa tiba na uboreshaji miundombinu ya huduma.

CRDB YAKABIDHI HOSPITALI YA HAYDOM MASHUKA 100

Benki ya CRDB imetoa msaada wa mashuka 100 kwenye hospitali ya rufaa ya Haydom Wilayani Mbulu Mkoani Manyara, kwa lengo la kuwasaidia wagonjwa wanaolazwa katika hospitali hiyo inayohudumia zaidi ya watu wa mikoa minne nchini.

Akizungumza wakati akikabidhi mashuka hayo 100 kwa mkurugenzi wa hospitali hiyo Dk Emanuel Nuwass, Meneja wa CRDB Tawi la Babati Ronald Paul alisema wanatoa msaada huo ili kurudisha hisani kwa jamii.

Paul alisema wamekabidhi mashuka hayo ili kutoa asante kwa jamii kwenye wiki ya huduma kwa wateja, kwa kurudisha kwao kile kidogo wanachopata kwa ajili ya kuboresha mahusiano zaidi baina ya benki hiyo na wateja wake.

“Tutaendelea kushirikiana na kusaidiana kwenye masuala mbalimbali ya kijamii kwani tunatambua jitihada na changamoto ya hospitali ya Haydom ambayo inatoa huduma kwa watu wa Manyara na waliopo mikoa ya jirani,” alisema.

Hata hivyo, mkurugenzi wa hospitali hiyo Dk Emanuel Nuwass alisema hii ni mara ya tatu kwa benki hiyo kutoa msaada kwenye hospitali ya Haydom, hivyo iendelee kuwa karibu nao kwa ajili ya kupeana ushirikiano wa kusaidia jamii.

Dk Nuwass alisema awali benki hiyo ilitoa mchango wa maendeleo wa sh1 milioni kwa ajili ya siku ya Haydom, kisha wakawapa zawadi ya ng’ombe mmoja mkubwa wa siku ya familia na mashuka 100 yatakayotumiwa na wagonjwa.

Alisema hivi karibuni bodi ya hospitali hiyo ilikubaliana na mpango wa malipo kwa wagonjwa kupitia njia ya kadi ya CRDB na zoezi hilo linatarajia kuwarahisishia watu wote watakaopata huduma katika eneo hilo la Haydom.

Kwa upande wake, meneja masoko mwandamizi wa benki hiyo Fredrick Siwale alisema benki hiyo itandelea kutoa huduma nzuri kwa wateja wao huku ikiboresha maeneo ambayo huduma haipatikani kwa kuhakikisha wanakuwepo.

“Kupitia kauli mbiu yetu ya ulipo tupo kama hatupo tutakuja na kama hatujaja utusubiri, tunalenga kuwahudumia watanzania wote na kupitia hilo ndiyo sababu tukafika kutoa mashuka haya kwani tunaithamini jamii,” alisema Siwale.

CRDB YATOA MIKOPO YA SH16.1 BILIONI MKOANI MANYARA

Benki ya CRDB Tawi la Babati Mkoani Manyara, imefanikiwa kutoa mikopo ya sh16.1 bilioni kwa wajasiriamali, watumishi wa Serikali, watumishi wa sekta binafsi, vyama vya kuweka na kukopa na asasi za fedha.

Watumishi wa serikali na wasekta binafsi 1,604 walikopeshwa sh12.8 bilioni na wajasiriamali 84 walikopa sh3.3 bilioni ikiwa ni pamoja na wafanyabiashara na wakulima.

Meneja wa benki ya CRDB Tawi la Babati, Ronald Paul akizungumza kwenye kilele cha wiki ya huduma kwa wateja, alisema wamedhamiria kuwapa wateja wao huduma bora na kuwanyanyua kiuchumi.

Paul alisema kwa muda wa miaka miwili tangu waanzishe huduma ya benki hiyo mkoani Manyara, wamefanikiwa kufungua matawi mengine madogo wilaya za Mbulu, Hanang, Simanjiro na Kiteto.

Alisema pia wamefanikiwa kufungua huduma za matawi madogo yaliyopo Magugu, Haydom na Mirerani ambayo kupitia hayo wameweza kupata akaunti za halmashauri za wilaya.

Alisema kwenye matawi yao madogo wamefanikiwa kuwa na huduma za ATM ambazo wamefungua 10 kwenye mkoa huo na zinafanya kazi kwa muda wa saa 24.

"Kwa kipindi hiki tumefanikiwa kuongeza ajira kwa watanzania hususani kwa wana Manyara kutoka wafanyakazi 12 hadi 37 kutokana na matawi mengine madogo yaliyofunguliwa katika wilaya mbalimbali," alisema.

Alisema wamefanikiwa kupata amana za sh11 bilioni zilizotokana na wateja 12,000 waliofungua akaunti za akiba, watoto jumbo, akaunti za malkia, akaunti maalum, bidhaa nyingi za kibenki za Simbanking, ATM na fahari huduma.

Mkurugenzi wa mji wa Babati Fortunatus Fwema alitoa wito kwa benki hiyo kuwatafutia wateja wa mbaazi wa nje ya nchi kwani hivi sasa wakulima wengi wanapata changamoto ya soko la zao hilo.

Fwema alisema kutokana na benki hiyo kutoa huduma za fedha hadi nje ya nchi hasa nchini India, wangetumia fursa hiyo kwa kuwaunganisha wakulima hao moja kwa moja na soko la mbaazi ambalo wanunuzi wengi hutoka nchini India.

Thursday 6 October 2016

BENKI YA CRDB YAKABIDHI MSAADA WA MADAWATI 200 MBULU



Benki ya CRDB Mkoani Manyara, imetoa msaada wa madawati 200 kwa halmashauri ya mji wa Mbulu kwa ajili ya kutumika kwenye shule za msingi, kwa lengo la kuhakikisha tatizo la madawati linamalizika katika eneo hilo.

Akizungumza wakati akikabidhi madawati hayo, meneja wa CRDB Tawi la Babati, Ronald Paul alisema katika kuazimisha wiki ya huduma kwa wateja wamejitolea msaada huo wa madawati hayo 200 kama mchango wao kwa jamii.

Paul alisema benki hiyo ya CRDB imetoa madawati hayo 200 ambayo yatagawanywa kwa wanafunzi wa shule tano za halmashauri ya mji wa Mbulu, ambapo kila moja ya shule hizo zitatolewa madawati 40.




“Tukiwa kwenye wiki ya huduma kwa wateja tunahakikisha tunarudisha kile kidogo tunachopata kupitia jamii, sisi tutaendelea kutoa mchango wetu kwa jamii ili kuhakikisha tunaunga mkono suala zima la maendeleo,” alisema Paul.

Alisema kwa muda wa miaka miwili tangu CRDB ianze kutoa huduma zake katika mkoa wa Manyara, wananchi wa mji wa Mbulu wamechangamkia fursa ya uwepo wao, kwa kuweka fedha, kutoa na kuchukua mikopo ya benki hiyo.




Mkurugenzi wa mji wa Mbulu Anna Mbogo akizungumza wakati akipokea madawati hayo aliushukuru uongozi wa CRDB kwa kutoa msaada huo kwani utawasaidia wanafunzi wa shule hizo kusoma kwa ufasaha.

Mbogo alisema awali walikuwa na upungufu wa madawati 3,179 ila walijitahidi na kuhakikisha madawati hayo yanapatikana na hadi sasa wana madawati 999 ya ziada ambayo yamehifadhiwa kwa ajili ya kutumika baadaye.

Hata hivyo, alitoa ombi kwa CRDB kuendelea kutoa msaada wa miundombinu ya shule za eneo hilo kwani hivi sasa wana mpango wa kujenga madarasa mengine ya shule ya msingi Imboru, yenye madarasa mawili pekee.

“Awali wanafunzi wa shule hii walikuwa wanatembea umbali mrefu wa kilometa tatu kutoka nyumbani hadi shuleni kila siku hivyo ili kukomesha hali hiyo kwa watoto hawa wadogo ndipo tukaamua kuijenga,” alisema Mbogo.

Alisema lengo lao ni kuhakikisha wanaendelea kuiboresha shule hiyo mpya kwa kujenga madarasa mengine zaidi ili baada kwani hivi sasa wanafunzi hao wanapata elimu kwa urahisi kwa sababu ipo karibu na makazi yao.