Tuesday 8 May 2018

MAHAWE AKABIDHI MASHUKA 20 MIRERANI

 Mbunge wa viti maalum wa Mkoa wa Manyara, Esta Mahawe amemkabidhi mashuka 20 Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na  watu wenye ulemavu) Jenista Mhagama, yatakayotumika na wanawake waliojifungua kwenye jengo la mama na mtoto katika kituo cha afya Mirerani Wilayani Simanjiro.

Akizungumza wakati akikabidhi mashuka hayo Mahawe alisema amejitolea kutoa mashuka hayo kwa lengo la kuwafunika wanawake watakaojifungua watoto wao kwenye kituo hicho cha watoto.

Alisema mashuka hayo yatakuwa alama ya upendo kwao kwa wanawake na watoto watakaokuwa wanajifunika pindi watakapokuwa wanapata huduma ya kujifungua kwenye jengo la mama na mtoto la kituo cha afya Mirerani.

“Pamoja na hayo mheshimiwa Waziri tunaomba kituo cha huduma za Ukimwi ambacho umeweka jiwe la msingi leo hapa Mirerani kijengwe pia kule machimboni ambacho kwa kiasi kikubwa kitawasaidia vijana wetu wanaochimba madini ya Tanzanite,” alisema Mahawe.
Hata hivyo, Waziri Mhagama alimpongeza Mahawe aliyejitolea mashuka hayo 20 na yeye akaahidi kutoa mashuka 100 yatakayotumika kwa wanawake watakaojifungua kwenye kituo cha afya Mirerani.

“Pia mbunge mwingine wa viti maalum wa mkoa wa Manyara, Martha Umbullah naye ameahidi kutoa mashuka 50 kwa ajili ya wanawake na watoto, hivyo wanaume nao wanunue mashuka ambayo watajifunika wanaume pindi wakifika kutibiwa kwenye kituo hicho cha afya,” alisema Waziri Mhagama.


Pia ili kuunga mkono zoezi hilo, Kaimu Katibu Tawala wa mkoa wa Manyara Misaile Mussa kupitia ofisi yake aliahidi mashuka 50 na Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) Mkoa wa Manyara, Mosses Komba aliahidi kujitolea mashuka 20.

No comments:

Post a Comment