Tuesday 8 May 2018

WAZIRI MHAGAMA AWEKA JIWE LA MSINGI KITUO CHA HUDUMA ZA UKIMWI MIRERANI

 Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na  watu wenye ulemavu) Jenista Mhagama amewataka wakazi wa mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, kukitumia ipasavyo kituo cha huduma za ukimwi ili kupunguza maambukizi mapya ya virusi vya ukimwi (VVU).

Mhagama aliyasema hayo mji mdogo wa Mirerani wakati akiweka jiwe la msingi wa kituo cha huduma za ukimwi kitakachotoa huduma kwa zaidi ya watu 49,000.


Alisema wananchi wa eneo hilo na wilaya za jirani na Mirerani wanapaswa kutumia huduma zitakazotolewa na kituo hicho ili kuhakikisha hakutakuwepo na maambukizi mapya ya VVU.

Alisema serikali imeonelea kuwa ni vyema kujenga kituo hicho cha huduma za Ukimwi kutokana na kasi ya maambukizi ya VVU kwani ni eneo ambalo linaongoza hivyo kuwa tishio japo mkoa huo una asilimia ndogo ya maambukizi. 
  
Aliwataka viongozi na wananchi wa eneo hilo kubadilisha kwa kukitumia kituo hicho cha huduma za Ukimwi ili miaka ijayo kuwe na mabadiliko makubwa ya VVU pindi upimaji ukifanyika upya.

"Wanaume msiwaache wanawake wenyewe wapime kwani mnapaswa kupima wote ili mtambue afya zenu zikoje ili kama kuna aliyeambukizwa aanze kupata ushauri na kutumia dawa," alisema Mhagama.

 Mkuu wa wilaya ya Simanjiro mhandisi Zephania Chaula akizungumza kwa niaba ya mkuu wa mkoa huo Alexander Mnyeti alisema bado maambukizi ya VVU yapo chini kwa Manyara.

Mhandisi Chaula alisema hali ya maambukizi kwa mkoa huo ni asilimia 2.3 ambapo halmashauri ya mji wa Mbulu maambukizi yapo chini kwa asilimia 0.64 na wilaya ya Simanjiro inaongoza kwa asilimia 2.85.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Simanjiro Yefred alisema hadi jengo hilo la kituo cha huduma za ukimwi linalojengwa na wataalamu wa Suma JKT litakapokamilika litagharimu kiasi cha sh492.5 milioni.

Myenzi alisema awamu ya kwanza ya ujenzi wa kituo hicho, halmashauri ya wilaya imechangia sh51.5 milioni kutokana na mapato ya ndani na kinatarajiwa kukamilika Juni 22 mwaka 2018.

Alisema wilaya imeweka uzito wa kipekee kwenye maeneo hatarishi ikiwemo mji mdogo wa Mirerani uliokuwa na asilimia 16 ya maambukizi ya VVU mwaka 2015 ila hadi Desemba 2017 imeshuka hadi asilimia 6.4.

"Mikakati inayotumika Mirerani ili kupunguza maambukizi mapya ni kuendelea na uhamasishaji wa jamii kwa kutumia washauri rika na wataalamu wa idara ya afya, kugawa mipira ya kiume ya kujikinga, upigaji na utoaji wa dawa za kufubaza VVU," alisema Myenzi.

Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya kudhibiti Ukimwi (TACAIDS) Dk Leonard Maboko alisema mradi huo umetokana na jitihada za pamoja kati ya TACAIDS, uongozi wa mkoa wa Manyara na wilaya ya Simanjiro.

Dk Maboko alisema alifanya ziara mji mdogo wa Mirerani Desemba 19 mwaka 2016 na kubaini kasi ya maambukizi ya VVU ilikuwa juu kutokana na shughuli mchanganyiko za kiuchumi na mwingiliano wa watu.

Mkazi wa mji mdogo wa Mirerani, Jafari Matimbwa alisema kituo hicho kitakuwa msaada mkubwa kwa jamii ya eneo hilo ambayo hivi sasa elimu ya maambukizi ya VVU inatolewa ipasavyo.

Matimbwa alisema kutokana na kutolewa kwa elimu hiyo wananchi wengi wanatambua namna ya kujikinga na maambukizi mapya na umuhimu wa kupima afya zao tofauti na awali.


No comments:

Post a Comment