Thursday 30 October 2014

WACHIMBAJI WALIA NA TANZANITEONE


Wachimbaji wadogo wa madini ya tanzanite katika mji mdogo wa Mirerani wilayani Simanjiro wameishtaki kampuni ya TanzaniteOne kwa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini wakidai kuwa imevamia na kupora baadhi ya migodi na zana za kufanyia kazi na kuharibu miundombinu yake.
 
Wakizungumza juzi na kamati hiyo iliyotembelea na kushuhudia baadhi ya migodi iliyoko Kitalu B (Opec), wachimbaji hao walidai kuwa wafanyakazi wa TanzaniteOne waliwavamia na kudai kuwa wanachimba kwenye eneo lao.

Meneja wa mgodi wa Deo Minja uliopo Opec, Omary Mandari alisema Septemba 8, mwaka huu, walivamiwa na watu hao waliopora tochi 38, nyaya za mita 1,000, diga tatu, huli 300 na wakakata mipira ya kupitisha upepo yenye mita 600.

“Tunadiriki kusema kampuni iliidharau kamati hii. Mlitoa agizo kuwa suala hili lisitishwe mpaka hapo mtakapotembelea eneo hili, tunashangaa hawakutekeleza badalika yake wakaamua kutuvamia na kufanya ukatili na uharibifu,” alisema Mandari.

Mmoja wa wamiliki wa mgodi katika eneo hilo, Mohamed Karia alidai kuwa walinzi wa kampuni hiyo waliingia mgodini kwake na kupora mashine mbili za kuchorongea na kuwajeruhi wafanyakazi wake kwa kuwapiga.

Mbunge wa Jimbo la Simanjiro, Christopher Ole Sendeka alisema mgogoro wa wachimbaji hao na TanzaniteOne unatokana na eneo hilo kugawanywa kisiasa, kwani wachimbaji hao ni wengi lakini wamepewa eneo dogo la mita 50 kwa 50.

“Wachimbaji wadogo walianza kuchimba tangu miaka ya 90. Mwaka 2004 wakaambiwa kuna sheria ilishatungwa na kutakiwa kila mmoja achimbe kwenye eneo lake, ndiyo ukawa mwanzo wa tatizo,” alisema Ole Sendeka.

Mwenyekiti wa kamati hiyo, Victor Mwambalaswa alisema watashughulikia tatizo hilo.la wachimbaji hao ambao wamekuwa wakilalamikia kila wanapokutana na viongozi wao wanapowafuata Bungeni mjini Dodoma.

“Kwa sababu tumeshuhudia tatizo hili hapa mgodini kesho (jana) tutakutana na viongozi wa wachimbaji wadogo wa Marema ili kutoa uamuzi wetu sisi kama Kamati ya Bunge kuhusu tatizo hili ambalo ni la muda mrefu sasa,” alisema Mwambalaswa.

Hata hivyo, Ofisa Uhusiano wa Kampuni ya TanzaniteOne, Halfan Hayeshi alisema walinzi wa kampuni hiyo hawajawahi kuingia kwenye mgodi wowote wa mchimbaji mdogo na kufanya tukio lolote lile la kiuhalifu.

“Sisi tunafanya kazi kwenye maeneo yaliyopo katika kitalu chetu cha C ila hizo habari za kudai kwamba tumeingia eneo la migodi ya wachimbaji wadogo siyo za kweli, hatuwezi kufanya kitendo kama hicho,” alisema Hayeshi.

Thursday 23 October 2014

WAZAZI KITETO WAZALISHWA KWA KUTUMIA MIFUKO YA PLASTIKI K



Kwa hisani ya gazeti la Mwananchi la Alhamisi ya Octoba 22 mwaka 2015

Joseph Lyimo, Mwananchi

Kiteto.Ukistaajabu ya Mussa utayaona ya Firauni. Haya ndiyo yanayojiri katika Wilaya ya Kiteto, mkoani Manyara ambako baadhi ya wakunga wa jadi huvaa mifuko ya plastiki maarufu kama ‘rambo au malboro’, mikononi ili kuwahudumia kina mama wakati wa kujifungua.

Awali wakunga hawa ambao hufanya kazi hii pasipo malipo yoyote rasmi, walikuwa wakizalisha wajawazito bila ya kuvaa chochote, lakini walianza kutumia aina hiyo ya ‘kinga’, baada ya wenzao wawili kuambukizwa Virusi vya Ukimwi.

Rose Mary Loshiye, ambaye pia ni mkunga wa jadi, anasema: “Wakunga wa jadi walikuwa wakiwazalisha wanawake wa jamii ya wafugaji bila kuvaa mipira mikononi na baadhi yao waliambukizwa Ukimwi, kwa hiyo tangu wakati huo hakuna anayethubutu kuzalisha akiwa mikono mitupu.

“Ikiwa hawana mipira ya kuvaa mikononi wanatumia mifuko ya plastiki, wanajifunga mkononi halafu wanatoa huduma hiyo kwa wakinamama.”

Wilaya hii inakaliwa zaidi na jamii ya wafugaji na huduma za afya na tiba zikipatikana umbali wa kati ya kilometa 45 na 50, hali ambayo inawapa wakunga wa jadi nafasi muhimu ya kuwa wahudumu pekee kwa wanawake wanaojifungua hasa nyakati za usiku.

Huduma ya afya kwenye Wilaya ya Kiteto yenye kata 19 na vijiji 59, ni changamoto kubwa kwani haikidhi matakwa ya sera ya taifa ya afya ya 2007 inayotaka kila kata iwe na kituo cha afya na kila kijiji kiwe na zahanati.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo, Bosco Ndunguru anasema Kiteto yenye kilometa 16,685 za mraba, ina hospitali moja ya wilaya na vituo viwili tu vya afya kati ya 15 vinavyohitajika na ina zahanati 15 kati ya 59 zinazotakiwa.

Kwa mujibu wa sensa ya watu na makazi ya 2012, Kiteto ina watu 244,669 wakiwemo wanaume 120,233 na wanawake 124,436 na ongezeko la watu ni wastani wa asilimia 6.1 kwa mwaka na kila kaya ikikadiriwa kuwa na wastani wa watu watano.

Vifaa kwa wakunga

Mkunga wa jadi wa Kijiji cha Bwagamoyo wilayani humo, Amina Malekela (56) anasema tatizo kubwa ni uhaba wa vifaa na kwamba wanapouliza sababu za kutopatiwa vifaa hivyo, wanaelezwa kuwa hawatambuliwi na hawapaswi kusaidia kuzalisha.

“Mara nyingi wanawake wengi hujifungulia nyumbani kupitia wakunga wa jadi ambao wanatumia mikono mitupu kuzalisha, kwani mipira ni tatizo haipatikani,” anaeleza Malekela.

Anasema kwa kuwa matukio hayo huwa ya ghafla, wakunga hushindwa kuvaa hata hiyo mifuko ya plastiki ambayo hutumia kwa ajili ya kujikinga na maambukizi ya VVU na kwamba ndiyo sababu wenzao wawili waliambukizwa.

Mratibu wa afya ya uzazi na mtoto wilayani Kiteto, Helena Batroba alithibitisha wakunga wawili wa jadi kufikishwa hospitalini wakidaiwa kuwa na maambukizi ya VVU.

“Kuna wanawake wawili ambao mwaka 2010 walikuwa wanatibiwa hapa hospitali ya wilaya, wakiwa na virusi vya Ukimwi na tulipouliza tukaelezwa kuwa ni wakunga wa jadi, ila sikumbuki walikuwa wametoka maeneo gani, mmoja alikuwa na miaka 70 na mwingine miaka 65,” anasema Batroba.

Kwa upande wake, Loshiye anasema licha ya kwamba hawana vifaa vya kazi hiyo, wamekuwa wanafanya kazi yao bila kulipwa chochote, kwani wanafanya hisani.

Anaeleza kwamba wakunga wa jadi hawana gharama kubwa kwa kuwa hupatiwa asante ya mdomo na wao huridhika kwa moyo mmoja na wakati mwingine hupewa kanga, vitenge na karanga.

Loshiye anasema wengine huridhika kwa kupata sifa wanapozalisha wanawake salama bila madhara yoyote.

Diwani wa Kata ya Magungu, Daudi Mwedimwage anasema wakunga wa jadi wanategemewa na wanawake wengi wajawazito katika kuwazalisha kutokana na huduma za afya kuwa mbali na kata hiyo.

“Kutoka hapa Magungu hadi Kibaya makao makuu ya wilaya ambapo kuna hospitali kilomita 55, na kutoka Magugu hadi kule Makawa wilayani Kongwa mkoani Dodoma ni kilomita 45, hivyo inakuwa vigumu jamii kupata huduma za afya kutokana na umbali,” anasema Mwedimwage.

“Kwa hiyo ni kweli kwamba wakunga wa jadi wanatumia mifuko ya malboro kwa ajili ya kupokea watoto wakati wa kuzalisha na hiyo inatokana na ukosefu wa vifaa vya kitaalamu, hivyo inawabidi watumie namna za kienyeji kwa ajili ya kujinusuru na maambukizi ya virusi vya Ukimwi kwani hawana namna nyingine.”
Hospitali ni gharama

Mkazi wa Kijiji cha Partimbo wilayani humo, Paulina Kimani (39) anakiri kwamba huzalishwa na wakunga wa jadi kutokana na ukubwa wa gharama za kujifungua kwenye hospitali ya wilaya hiyo ambazo ni kuanzia Sh20,000.

“Tunashindwa kuchangia hizo fedha tunazoelezwa kwamba ni za nyembe, gloves (mipira ya kuvaa mikononi), mpira wa kunyonyea uchafu na mpira wa kulalia wakati wa kujifungua,” anasema Kimani.

“Pia hao wahudumu wana lugha chafu, ni tatizo kwa mtoto mdogo anakwambia wewe mama hadi umri huu bado unazaa tu achia watoto wako au wajukuu wako. Unapenda starehe hadi umri huo?”

Hata hivyo, kaimu mganga mkuu wa Wilaya ya Kiteto, Dk Leadry Malisa alikanusha wanawake wajawazito kutakiwa kutoa fedha kwa ajili ya kulipia huduma ya kuzalishwa kwenye hospitali au vituo vya afya na kwamba huduma hizo hugharamiwa na Serikali.

Dk Malisa anakiri upungufu wa vifaatiba, pia vifaa vya kujifungulia kwa wanawake wajawazito, kutokana na mgawo mdogo unaotolewa na Bohari Kuu la Dawa (MSD) na hiyo ni changamoto inayowakabili kwa muda mrefu wilayani humo.

“Suala la uchache wa mipira ya kuvaa mikononi (gloves) ni tatizo, haitoshi, hivyo tunawaomba kina mama hasa wa jamii ya wafugaji, wakikaribia kujifungua, wajiandae mapema kwa kusogea karibu na huduma za afya, ili wapate huduma sahihi wakati wa kujifungua kuliko hivi sasa wanapojifungulia nyumbani mwao kwa msaada wa wakunga wa jadi,” anaeleza Dk Malisa.

Kwa upande mwingine, mratibu wa afya ya uzazi na mtoto, Batroba anasema si kweli kwamba wauguzi katika sehemu za kutoa huduma za afya wanatoa lugha zisizo rafiki kwa wanawake wajawazito na kwamba kuna uadilifu mkubwa.

“Hata hivyo, tutachunguza suala hili kama kweli lipo, ila tumekuwa tukifuatilia jambo hili kwa wauguzi wetu na tumebaini kwamba lugha wanayotumia ni ya kitaalamu na siyo lugha ya matusi kama wanavyofikiri baadhi ya wanawake hao,” anasema Batroba.

Wakunga watetewa Katibu wa tiba asilia na tiba mbadala wa Wilaya ya Kiteto, Muya Kisairo anasema wakunga wa jadi ni muhimu wilayani humo kwani wamekuwa wakitoa huduma za uzazi, lakini Serikali ni kama haiwatambui kwa na hivyo haiwapi vifaa.

Kisairo anasema wilaya hiyo ina zaidi ya wakunga 100 wa jadi ambao wapo katika vijiji mbalimbali na kila kijiji kinawategemea katika kuwapa huduma wanawake tangu wakiwa wajawazito, kwa kuwa wengi wao wanashindwa kwenda kliniki au hospitalini kutokana na umbali.

Anaeleza kwamba utendaji kazi wa wakunga wa jadi wilayani humo ni mzuri isipokuwa tatizo ni ukosefu wa vifaa kwani baadhi ya maeneo ya vijijini hadi ufike kwenye huduma za afya, inakubidi utembee umbali wa maili 10 au zaidi, hivyo shughuli zote za uzalishaji wanafanya wakunga wa jadi.

“Upungufu wa vifaa tiba ni tatizo sana kwa wakunga wa jadi wa Wilaya Kiteto ambao ni wakombozi wa jamii linapokuja suala la uzazi, kwani wanatumia mifuko ya rambo kutokana na ukosefu wa mipira ya kuvaa mkononi,” anasema Kisairo.

Tuesday 14 October 2014

MGOGORO MACHIMBO YA MADINI YA TANZANITE MIRERANI



Mussa Juma, Mwananchi

Mirerani. “Sheria hii inatumika kwenye machimbo ya dhahabu na almasi siyo tanzanite ambayo inachimbwa kwa kufuatwa miamba,” anasema Mnenei.

Anasema kwa kutaka kusimamia sheria hiyo ni kutaka kuwaondoa wachimbaji wadogo, Mererani kwani kwa jinsi walivyopewa maeneo yao hakuna hata mmoja ambaye anachimba ndani ya leseni.

“Kuwaondoa wachimbaji hapa ni kusababisha maafa kwa familia zao na taifa zima kwani watu zaidi ya 10,000 wakikosa kazi, sijui wao na familia zao watategemea nini,” anasema Mnenei na kuisihi Serikali kutatua mgogoro huo.

Papa King Mollel ni mmoja wa wachimbaji wadogo, maarufu Mkoa wa Arusha, anasema sheria hiyo ya madini na gharama kubwa za zana za uchimbaji ni kikwazo kwa wachimbaji wadogo.

“Ni kweli migodi mingi imesimama, lakini tatizo ni sheria na gharama za uchimbaji pia ni kubwa kwa sasa tofauti na miaka ya nyuma,” anasema.

Mbunge wa Simanjiro, Christopha Ole Sendeka anafafanua kuwa kimsingi sheria ya uchimbaji madini ya vito, ipo wazi kuwa madini hayo yatachimbwa na wazawa pekee sasa kuwa na sheria na kutetea mwekezaji ni kuvunja sheria pia.

“Msimamo wangu hautabadilika ni muhimu kuifanyika marekebisho sheria ya uchimbaji madini ya vito, ili iendane na wakati na sheria iliyopo sasa haitekelezeki,” anasema Sendeka.

Watafiti nao waeleza upungufu wa sheria

Amani Mustapha ni Mkurugenzi wa Shirika la Haki Madini, ambao wamefanya utafiti mbalimbali Mirerani, anasema sheria hiyo ya madini haitekelezeki na inalenga kuwaondoa wachimbaji wadogo Mirerani.

Anasema kwa sasa hakuna sababu za kulaumiana kwani, makosa yalifanyika tangu miaka ya nyuma kugawa machimbo ya Mirerani kisiasa na kutoa eneo moja kubwa kwa kampuni moja ya wawekezaji bila hata kuzingatia sheria ya madini.

Mustapha anasema ni muhimu busara kufuatwa, kwani wachimbaji wadogo wote zaidi ya 10,000 eneo lao halifikii eneo la mwekezaji mmoja.

“Binafsi nilikuwa mmoja wa wajumbe walioambatana na wachimbaji Dodoma kuonana na Kamati ya Bunge na tulieleza tatizo hilo kwa mapana na ambalo linasabisha sasa migodi mingi kusimama,” anasema.

Anasema kwa mapendekezo yake, ni busara sheria kutazamwa upya pia kupunguza eneo la mwekezaji ili wachimbaji wadogo wachimbe kwani wengi maisha yao yanategemea Mirerani.

“Ukiwaacha watu zaidi ya 10,000 bila ajira kwa kumlinda mtu mmoja, tutarajie matukio mengi ya ajabu mijini na ongezeko la uhalifu,” alisema.

Alisema machimbo ya Mirerani yanategemewa na zaidi ya watu 40,000 wa Wilaya ya Simanjiro na Mkoa wa Arusha, hivyo kuwabana wachimbaji wadogo kutakuwa na athari kubwa kama ambazo zimeanza kuonekana sasa kuzorota kwa uchumi wa Mirerani.

Mustapha anasema kutokana na majibu ya Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo kwa wachimbaji wadogo muafaka hadi sasa haujapatikana na suala hili sasa limepelekwa kwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda.

Mchimbaji Ismail Kaaya anasema pia kupewa mwekezaji mmoja kumiliki eneo la kilomita za mraba 7.6 ni makosa kwa mujibu wa kanuni za uchimbaji madini ya vito aya ya 5(1)(f) ambayo inasema ukubwa wa mwisho wa eneo utakuwa kilomita moja ya mraba.

“Pia hata hii sheria ambayo imesababisha migodi kufungwa ilikuwa haituhusu sisi kwani imetungwa wakati tayari tumekuwa tumeingia chini eneo hilo la mwekezaji kwa kuwa hakukuwa na sheria za kuzuia kutoingiliana chini ya migodi,” anasema.

Lusekelo Mwakalukwa ni mmoja wa wanasheria wa Kampuni ya Tanzanite One, anaeleza uvamizi ambao unafanywa na wachimbaji wadogo katika migodi ya Tanzanite One ni kukiuka sheria na umesababisha madhara kadhaa kwa wafanyakazi.

Hali ya uchimbaji Mirerani

Ofisa madini ambaye ni mtaalumu wa miamba (jiologist) Mererani, Mithayo Fransis kati ya migodi 551 inayochimbwa katika maeneo ya kitalu B na D ni migodi isiyozidi 120 ambayo ndiyo inachimbwa kwa sasa. 

Hata hivyo, anasema licha ya sheria hiyo, lakini kuna matatizo mengine yanayochangia kusimamishwa uchimbaji hasa ni gharama kubwa za uchimbaji kwa sasa kutokana na migodi mingi kufika umbali mrefu.

“Ndiyo sababu sasa hata wafanyakazi wamepungua sana mgodi ambao ulikuwa una vijana kati ya 200 hadi 100 sasa una vijana 15 tu, kwani kuna migodi imeanza kutumia zana za kisasa katika kutoa nje michanga tofauti na zamani kutumia watu,” anasema.

Anapinga pia hoja kuwa madini mengi yapo, eneo la mwekezaji kitalu C kwa maelezo kuwa mserereko wa miamba ya madini haiwezi kuwa sawa kwa migodi ya kitalu B na D yote kudai miamba inaelekea kitalu C.

Maelezo ya Wizara ya Nishati na Madini

Kamishna wa Madini Kanda ya Kaskazini, Alex Magayane licha ya kukiri siasa ndiyo ilivuruga ugawaji wa vitalu Mirerani, lakini anasema ni muhimu sheria kufuatwa.

Anasema siyo kweli kuwa wizara ilitunga sheria hiyo, kumlinda mwekezaji kwani sheria ilikuwepo tangu mwaka 1998 na kilichofanyika mwaka 2004 na 2010 ni kuitafrisi vizuri sheria.

Magayane anafafanua kuwa haiwezekani mtu mwenye leseni ya madini kuchimba madini nje ya leseni, kwani jambo hilo halipo duniani na hakuna ukiukwaji wa sheria kutokana na msimamo wa wizara hiyo.

Anasema ni kweli kuwa kugawa migodi kwa mita 50 kwa 50 ilikuwa ni makosa kwani eneo hilo, huwezi kuchimba madini na ni kinyume cha sheria.

Magayane anasema tatizo na uchimbaji kwa wachimbaji wengi wadogo siyo endelevu kwani wamekuwa wakutumia fedha nyingi kufuata eneo ambalo wamepata taarifa kuna madini bila kujali ukubwa wa leseni.

“Ni kweli migodi mingi ipo ndani ya eneo la mwekezaji Tanzanite One na ndiyo sababu tulitaka kuifunga migodi 19 na kuibua malalamiko na jambo hili ni la kisheria,” anasema.

Anasema pia inawezekana kufungwa kwa migodi mingi ya wachimbaji wadogo kunatokana na maeneo yao kuisha madini na hili lipo kwa migodi mingi nchini.

Nini kifanyike Mirerani kunusuru wachimbaji wadogo

Ili kutowaondoa maelfu ya wachimbaji wadogo Mirerani, Kamishna Mahayane anaungana na Waziri Muhongo, kuwashauri wachimbaji wadogo kuungana na kuunda kampuni moja ili wao na wawe wanagawana mapato.

Takwimu za wizara hiyo zinaonyesha kama wachimbaji 100 wenye hisa wakiungana kila mmoja anaweza kupata takriban Sh500 milioni kwa mwaka kutokana na makisio yaliyofanyika kwa mapato ya Dola 35 milioni kwa mwaka Mirerani.

Anasema kwa uchimbaji wa sasa unachochea migogoro na ni vigumu kuendelea kwa muda mrefu kwani kunahitajika teknolojia za kisasa zenye gharama kubwa kama wasipoungana.

Hata hivyo, ushauri huu ambao ni wa muda mrefu wa Serikali unapingwa na wachimbaji kwa maelezo ya tofauti kubwa ya uwekezaji katika migodi baina yao.

“Kuna mtu amewekeza zaidi ya Sh8 bilioni sasa kumwambia aanzishe kampuni moja na mtu ambaye hajawekeza hapa ni tatizo pia tunadhani hii ni njama tuungane tushindwe kuendesha kampuni migodi iuzwe kwa wawekezaji,” anasema John Mika.

Wachimbaji wadogo wao, ushauri mkubwa wanaotoa kwa Serikali ni kufuata mapendekezo ya Tume ya Jaji Mark Bomani na aliyekuwa Mkuu wa Majeshi Generali Robert Mboma ya Mei 2002 kuwa madini ya Tanzanite yachimbwe na wachimbaji wadogo pekee kwa kuwa hayana ushindani katika soko la kimataifa.

Tume hiyo Mboma pia ilipendekeza itatue tatizo la mipaka baina ya kitalu B na C na kurejesha wa mwanzo wa mwaka 1987 na Serikali isitiwe leseni katika eneo la kitalu C kwa mwekezaji mkubwa na iwawezeshe wachimbaji wadogo kuchimba madini hayo.

Nini kitatokea sasa ili kumaliza mvutano huu unaowaondoa wazawa kuchimba madini, tusubiri kwani jambo hili linatarajiwa kuwa ajenda kubwa kisiasa katika uchaguzi mkuu ujao Mkoa wa Manyara na Arusha.

MWISHO.

Sunday 12 October 2014