Wednesday 22 November 2017

DED KAMOGA AKIITUMIKIA HALMASHAURI YA WILAYA YA MBULU


 Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara, Hudson Starnley Kamoga akiwakabidhi ndoo yenye maji wanafunzi wa shule ya msingi Endamasak, baada ya mradi wa maji kukamilika na kuondoa tatizo la muda mrefu la ukosefu wa maji lililokuwa linawakabili wanafunzi na walimu wa shule hiyo.



Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara, Hudson Starnley Kamoga (kushoto) akikagua mabomba ya maji kwenye mradi wa Kijiji cha Endamasak, kulia ni mhandisi wa maji wa Halmashauri hiyo John Michael.



Mkurugenzi Mtendani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara, Hudson Starnley Kamoga akila makande kwenye shule ya msingi Endamasak, huku wanafunzi wengine wakipanga foleni ya kupata chakula hicho, baada ya kukamilika kwa mradi wa maji shuleni hapo.

NAIBU WAZIRI WA MADINI LADSLAUS NYONGO AWATAKA WAUZA VIFAA VYA UJENZI WA UKUTA KUTOPANDISHA VIFAA BEI

 Naibu Waziri wa Madini Ladslaus Nyongo amewataka wauzaji wa vifaa vya ujenzi wa ukuta unaozunguka migodi ya madini ya Tanzanite wa Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, kutowauzia wanajeshi bei ghali vifaa vinavyojengea ukuta huo. 

Nyongo aliyasema hayo alipotembelea mji mdogo wa Mirerani wakati wa ukaguzi wa ujenzi wa ukuta na eneo litakalofanyika mnada wa madini ya Tanzanite. 

  
Alisema shughuli za ujenzi wa ukuta ni za kujitolea siyo za biashara ya kupata faida hivyo wafanyabiashara wasitake faida. 

Alisema wafanyabiashara wanapaswa kutumia fursa ya ujenzi wa ukuta huo kwa kufanya biashara na kupata faida kidogo kuliko kuweka tamaa ya kuuza vitu bei ghali. 


"Rais John Magufuli wakati anazindua barabara ya lami ya Kia-Mirerani Septemba 20 mwaka huu alitoa agizo la kujengwa kwa ukuta kwa lengo la kulinda rasilimali hii adimu hivyo wafanyabiashara wasijinufaishe," alisema Nyongo. 

Aliwapongeza askari wa jeshi la kujenga Taifa kupitia shirika la Suma JKT kwa namna wanavyofanya shughuli hiyo ya kujenga ukuta kutokana na kasi iliyopo. 

Alisema ana imani kazi hiyo itachukua muda wa miezi sita kama Rais Magufuli alivyoagiza na wao kama wizara wataendelea kutoa ushirikiano kwa jeshi hilo. 
Awali, mkuu wa wilaya ya Simanjiro mhandisi Zephania Chaula alisema askari hao wanakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo ya magari yanayobeba vifaa vya ujenzi kusimamishwa na askari polisi wa usalama barabarani wa mkoa wa Arusha, hivyo kuwachelewesha kwenye ujenzi. 

Mhandisi Chaula alisema ili kuhakikisha hilo alifanyiki tena wameamua kuweka karatasi maalumu kwenye magari yanayobeba vifaa vya ujenzi wa ukuta huo ili wasisumbuliwe tena. 

Alisema walitoa taarifa ngazi ya mkoa wa Manyara ili wakutane na mkoa wa Arusha, kwa lengo la kuzungumza na kumaliza changamoto za ujenzi huo. 




MACHIMBO YA DHAHABU NYARUGUSU

 Mchimbaji wa madini ya dhahabu kwenye machimbo ya Nyarugusu Mkoani Geita, Christopher Kadeo akizungumza na wadau wa madini waliotembelea mgodi wake. 


LOWASSA AMNADI MGOMBEA UDIWANI MAKIBA NA KUKANUSHA KUTAKA KWENDA CCM

Waziri Mkuu mstaafu na mjumbe wa Baraza Kuu la Chadema, Edward Lowassa, amemshukia Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mrisho Gambo kuwa asitafute umaarufu wa kisiasa kwa kutumia jina lake. 

Akizungumza jana kwenye mkutano wa kampeni ya kumnadi Joyce Rutha (Chadema) mgombea udiwani wa kata ya Makiba Wilayani Arumeru Mkoani Arusha, Lowassa alisema hujatuma watu kwa Gambo ili arudi CCM. 

Alisema kuendelea kumzungumzia Gambo kwenye majukwa ya kisiasa ni kumpa umaarufu wa bure kwani yeye hujamtuma mtu au watu kutoka Monduli ili aende kwa mkuu huyo wa mkoa kwa lengo la kuomba arudi CCM. 


  
Mkuu wa mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo jana kwenye kurasa zake za mitandao ya kijamii ya Facebook, Instagram na tweeter, aliandika kuwa amepokea ujumbe kutoka Monduli. 

Gambo aliandika kuwa ujumbe huo ulikuwa na ombi moja kubwa amuombee mzee wa Monduli kwa Rais Magufuli ili akubali kumuona na yeye yupo tayari kurudi nyumbani kama Rais atakubali kumuona. 

Alisema ujumbe huo unasema ombi hilo katuma muda mrefu bila majibu. 

"Mnao mfahamu mzee huyu mfikishieni ujumbe kuwa salamu nitaifikisha,  mjumbe hauwawi," aliandika Gambo.

  
Lowassa alisema jana mchana alisoma kwenye mitandao ya kijamii kuwa ametuma watu wamuombee ili arudi CCM jambo ambalo siyo kweli. 

"Siwezi kumjibu huyu kijana kwani kuendelea kumjadili ni kumpa umaarufu hivyo simjibu chochote kwenye hilo," alisema Lowassa. 

Akizungumza wakati wa kumnadi mgombea udiwani huyo, Lowassa aliwataka wananchi wa kata ya Makiba kumpa kura nyingi za ndiyo Rutha ili awe diwani wao. 

"Mwaka 2015 nilikuja kuwaomba kura na mkanipa kwa wingi sasa endeleeni kuikataa CCM kwa kumpa kura mgombea wetu wa Chadema Rutho," alisema Lowassa. 

Pia, alisema wananchi zaidi ya milioni sita waliompigia kura nao wanapaswa kusemewa na wao kwa kuwepo kwa serikali ya mseto. 

Alisema katiba mpya ni jibu kwa kuweka kipengele cha serikali ya mseto kwa mlengo wa kushoto na kulia ili mtu mmoja asipate nafasi ya kuharibu vitu vingi. 

Alisema hata Marekani na Ufaransa wanashirikiana kwenye nafasi hizo pindi uchaguzi ukifanyika bila kujali chama ni cha kijamaa au kibepari. 

"Japo kuna wabunge lakini wale watu milioni sita walionipigia kura nao wanapaswa kuwakilishwa serikali kama wale milioni nane wengine ambao wana mawaziri, wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya, wakurugenzi na viongozi wengine," alisema Lowassa. 


 Mbunge wa jimbo la Arumeru mashariki Joshua Nassari alisema Makiba wanapaswa kumchaua Rutha kwani kuna Chadema inaendesha shughuli zake bila kujali ukabila ndiyo sababu tarafa hiyo ikapata Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Meru. 

Nassari alisema wananchi wanapaswa kumchagua Rutha bila kujali kabila lake kwani jambo la muhimu ni kusimamia maendeleo. 

Alisema Rutha ni mgombea mwadilifu kwani wapinzani wao waliweza kumrubuni kwa sh5 milioni na kumwekea pingamizi lakini tume ikamrudisha. 

"Kama hawamuogopi Rutha kwa nini wanamwekea vipingamizi wasije kwa debe, waje kwa debe tupambane wananchi waamue wenyewe, yule kijana aliuza utu wake kwa sh2 milioni lakini huyu sh5 milioni alizikataa," alisema Nassari. 
 Mbunge wa jimbo la Simanjiro James Ole Millya alisema ana imani kubwa na watu wa Makiba watampa kura nyingi Rutha ili awe diwani wao. 

Ole Millya alisema anashangazwa na watu waliokuwa Chadema kisha wanarudi CCM ili hali hakuna jambo kubwa walilofanyiwa hadi kusababisha kuachana na chama hicho zaidi ya tamaa. 

"Ni kwa furaha gani wewe Mollel unarudi CCM, ili hali wafugaji wanaendelea kuteseka kote Tanzania, jibu la yote hayo ni kuendelea kuwa Chadema na siyo kukimbia," alisema Ole Millya. 
 Mgombea udiwani wa kata hiyo Joyce Rutha alisema endapo atachaguliwa kuwa diwani, atahakikisha anakuwa mwakilishi mwema wa wananchi wa eneo hilo kwenye halmashauri ya wilaya hiyo. 


 Rutha alisema ataendelea kufanya kampeni ya nyumba kwa nyumba ili ahakikishe Chadema inashinda kwenye nafasi hiyo. 


WAANDISHI WA HABARI WA MANYARA NA ARUSHA

Waandishi wa habari wa Mikoa ya Manyara na Arusha wakiwa kwenye picha ya pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Mbulu Chelestino Mofuga baada ya kupata mafunzo ya namna ya kuandika maombi ya ruzuku kwa Tanzania Media Foundation (TMF) Mjini Babati.

Friday 10 November 2017

RC MNYETI ATEMBELEA UKUTA MIRERANI

  Mkuu wa Mkoa wa Manyara Alexander Mnyeti, ameanza rasmi kazi Mkoani humo kwa kukagua ujenzi wa ukuta unaozunguka migodi ya madini ya Tanzanite Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro, ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Rais John Magufuli. 

Mnyeti alitembelea eneo hilo na mwenyeji wake mkuu wa wilaya hiyo mhandisi Zephania Chaula na kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa huo. 

Alipongeza kasi ya maandalizi ya ujenzi huo kwani kila sehemu aliyokagua ambapo ukuta utapita aliwakuta vijana hao wa JKT wana ari na hamasa ya utendaji kazi. 

"Kwa namna vijana wetu wanajeshi wanavyoonekana kwenye maeneo yote niliyopitia wanaonyesha wataimaliza kazi hii ndani ya muda mfupi tofauti na agizo la miezi sita lililotolewa na Rais Magufuli," alisema Mnyeti.

Aliwaahidi kutoa ushirikiano kwa jambo lolote lile watakalokuwa wanalitaka kwenye serikali ili kuhakikisha agizo hilo la Rais Magufuli linatekelezeka kwa wakati husika. 
 Kamanda wa operesheni ukuta Mirerani, Kanali Festus Mang'wela alimhakikishia mkuu huyo wa mkoa kuwa vijana wote wanaojenga ukuta huo watafikishiwa ujumbe wa kujikinga na maambukizi ya VVU kwa lengo la manufaa ya kulinda afya zao. 

Kanali Mang'wela alisema ukuta huo  wenye kilometa 24.5 na urefu wa mita tatu kwenda juu umeanza kujengwa rasmi Novemba 6 mwaka huu. 

Alisema mkuu wa JKT Meja jenerali Michael Isamuhyo ndiye alikuwa mgeni rasmi kwenye uzinduzi huo wa ukuta wanaotarajia kuujenga kwa muda usiopungua miezi sita. 

Alitoa shukrani kwa serikali ya wilaya ya Simanjiro kwa ushirikiano mkubwa wanaowapa askari hao wakati wa utekelezaji wa ujenzi wa ukuta huo.
Katibu Tawala wa wilaya ya Simanjiro, Zuwena Omary akisoma taarifa ya Wilaya hiyo kwa mkuu wa mkoa huo alisema wanashirikiana ipasavyo katika maandalizi ya ujenzi wa ukuta huo. 

Alisema serikali ya wilaya ya Simanjiro na uongozi wa JWTZ wamekuwa na mawasiliano ya mara kwa mara ili kuhakikisha zoezi hilo linafanyika ipasavyo na kwa wakati muafaka. 

Alisema ukuta huo utachangia kudhibiti utoroshwaji wa madini hayo ambayo huuzwa yakiwa ghafi au kusanifiwa na kuuzwa na madalali na wanunuzi wa ndani na nje ya nchi. 

Alisema katika utekelezaji wa agizo la Rais Magufuli, wamefanikisha uanzishwaji wa ujenzi wa ukuta na kupatikana eneo la mnada wa madini ya Tanzanite Mirerani. 

"Hadi hivi sasa imeshafanyika minada minne ya madini ya Tanzanite jijini Arusha na serikali kuu na halmashauri ya wilaya ya Simanjiro zikapata kodi ya mapato na kodi ya huduma ila minada ijayo itafanyika Mirerani," alisema Omary. 


WACHIMBAJI WAKUTANA GEITA KUMNYANYUA ZAIDI MCHIMBAJI MDOGO

 Mkuu wa Mkoa wa Geita Robert Luhumbi amewataka wadau wa madini kuhakikisha sekta hiyo inaakisi maendeleo ya jamii inayozunguka eneo hilo ili waone faida ya kuwepo kwa rasilimali hiyo muhimu. 

Luhumbi aliyasema hayo mjini Geita kwenye ufunguzi wa majadiliano ya wachimbaji wadogo Tanzania yaliyowashirikisha wadau wa madini wa nchi mbalimbali duniani. 

Akizungumza kabla ya washiriki hao hawajaanza safari ya kutembelea migodi ya madini ya dhahabu, Luhumbi alisema faida ya uwepo. 
 Alisema uwepo wa rasilimali ya madini ya dhahabu mkoani Geita bado haujaonekana ipasavyo kwa jamii ya eneo hilo kwani zinapaswa kuboresha miundombinu mbalimbali ikiwemo ya barabara, maji, elimu, afya na mengineyo. 

"Hatutaki kuona rasilimali ya madini inaoneka kuwa ni laana kwa jamii badala ya baraka, kwani kupitia tunu hiyo wananchi wanapaswa kunufaika kwa kuona maendeleo yanafanywa kwenye maeneo hayo," alisema Luhumbi. 

Alisema sekta ya wachimbaji wadogo wa madini inafanywa na idadi ya watu milioni moja hadi milioni moja na nusu nchini hivyo wanapaswa kuwekewa mazingira rafiki yatakayoboeesha maisha yao. 

 Mkurugenzi wa asasi ya Haki Madini, Amani Mhinda alisema wameandaa mdahalo huo kwa uwezeshwaji wa taasisi ya kimataifa ya mazingira (IIED) kituo cha kimataifa cha utafiti wa misitu (CIFOR) na kampuni ya ushauri ya MTL. 

Mhinda alisema lengo ni kutoa suluhu juu ya changamoto zinazomkumba mchimbaji mdogo nchini na kupendekeza majawabu. 

Alisema sekta ya uchimbaji madini nchini ni kati ya sekta zinazokua kwa kasi kubwa na yenye mchango mkubwa wa uchumi wa Taifa. 

Alisema ingawa mipango mahususi ya kisera juu ya uchimbaji mdogo imeanzishwa, bado kuna changamoto nyingi hasa katika uelewa, ujasiri, mipango, fedha na taratibu zinazokwamisha utekelezaji wa sera na maboresho. 

 Mchimbaji wa madini wa kampuni ya Nsangano Gold mine, Renatus Nsangano alisema bado wachimbaji wadogo wana changamoto ya kufanya kazi bila kufanya utafiti. 

Nsangano alisema endapo wangekuwa wanafanya utafiti na kubaini madini yalipo ingekuwa na tija kubwa kwa wachimbaji wengi. 


Hata hivyo, alisema wamesaidia jamii zinazowazunguka kwenye masuala mbalimbali ya maendeleo ikiwemo ya elimu, afya na maji.