Monday 31 July 2017

MIGODI MIWILI YA GEM AND ROCK NA CT YA TANZANITEONE YAFUNGWA

Sakata la kifo cha mchimbaji wa madini ya Tanzanite wa mgodi wa Gem & Rock Venture wa mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, unaopakana na kampuni ya TanzaniteOne, limechukua sura mpya baada ya mgodi huo na ule wa CT kufungiwa. 

Takribani kwa muda wa siku tano mfululizo kulikuwa na vurugu zilizotokea kwenye migodi hiyo iliyopakana huku kila upande ukituhumu mgodi mwingine kuwa unawarushia mabomu ya kutengeneza kienyeji, kupitia mitobozano iliyopo.  

Kutokana na vurugu hizo mchimbaji wa mgodi wa Gem & Rock Venture, Lembris Mbatia (22) alifariki dunia na wengine 13 kujeruhiwa baada ya kudaiwa kupigwa bomu la kutengeneza kienyeji na kulipuliwa mgodini humo na wafanyakazi wa kampuni ya TanzaniteOne.  

Kamishna msaidizi wa madini kanda ya kaskazini, Adam Juma alisema amesitishwa shughuli za uchimbaji kwenye migodi hiyo miwili ili kupisha uchunguzi ufanyike juu ya mgogoro uliopo hivi sasa. 

Juma alisema wameamua kusitisha kwa muda shughuli za uchimbaji wa madini kwenye migodi hiyo miwili ili kufanyike mazungumzo baina ya pande hizo mbili na kufikiwe muafaka wa uchimbaji salama. 

Alisema wafanyakazi wa Wizara ya Nishati na Madini, kutoka kitengo cha ukaguzi wa migodi wanatarajia kufika kwenye eneo hilo na kukagua migodi hiyo miwili kwa lengo la kupata suluhu. 

Mkuu wa wilaya hiyo, mhandisi Zephania Chaula alizitaka pande hizo mbili kukaa pamoja na kupata ili kupata suluhu ya mgogoro huo ambao umesababisha kifo cha mchimbaji mmoja na wengine kujeruhiwa. 

"Pamoja na hayo, bado nasisitiza kutotumika kwa matumizi ya mabomu ya kutengeneza kienyeji kwani nimeshaagiza polisi wawachukulie hatua kali wale wote watakaobainika kuwa wanajihusisha na vitendo hivyo viovu," alisema mhandisi Chaula. 

Alisema suala la usalama katika migodini linapaswa kupewa kipaumbele kwani endapo kutatokea matatizo kwenye machimbo hayo ya Tanzanite, shughuli za uchimbaji hazitafanyika. 

Meneja wa mgodi wa Gem & Rock Venture, Joel Saitoti alisema ni kawaida ya wafanyakazi wa kampuni ya TanzaniteOne kuteka migodi mara baada ya kupata tetesi kuwa mgodi unaopakana nao unatoa madini. 

Saitoti alisema kampuni ya TanzaniteOne inavyofanya siyo jambo sahihi kwani ni migodi mingi ya wachimbaji wadogo ambayo imedhulumiwa haki zao kwa kuporwa njia zinazotoa madini. 

"Japo tumefungiwa kwa muda katika migodi yote miwili lakini wao TanzaniteOne wanaendelea na kazi kwenye migodi yao mingine na tunasubiri tukutane nao tuzungumze ili tupate suluhu," alisema. 

Hata hivyo, meneja wa ulinzi wa kampuni ya TanzaniteOne Abubakary Yombe alikanusha vikali wafanyakazi wa kampuni yake kutuhumiwa kumuua mchimbaji wa mgodi huo wa Gem & Rock Venture, Mbatia. 

Alisema wenyewe wanafanya kazi kwenye eneo la leseni yao ila wachimbaji wa mgodi wa Gem & Rock Venture ndiyo wamewaingilia katika mtobozano na kufanyia kazi sehemu ambayo siyo ya kwao. 


"Habari zinazotolewa kuwa tunateka migodi ya wachimbaji wadogo siyo za kweli kwani wao ndiyo wanaingia ndani ya eneo letu la leseni kupitia mtobozano na serikali inapaswa kuchukua hatua juu ya hilo ili kukomesha tatizo hilo," alisema Abubakary. 

No comments:

Post a Comment