Thursday 8 February 2018

WACHIMBAJI TANZANITE WATAKA UKUTA UWE NA MANUFAA NAO



WACHIMBAJI wadogo wa madini ya Tanzanite wa Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, wameiomba Serikali kuhakikisha nia ya kujenga ukuta unaozunguka migodi ya madini hayo unakuwa na manufaa kwao na maendeleo ya nchi.

Wakizungumza kwenye kikao cha wadau wa madini ya Tanzanite, wachimbaji hao wamedai kuwa nia ya kujenga ukuta isiwe kuwakandamiza wachimbaji wadogo ila kuhakikisha rasilimali hiyo inanufaisha Taifa.

Katibu wa chama cha madalali wa madini mkoa wa Manyara, Mohamed Mughanja alisema ukuta huo usibadili utaratibu uliozoeleka wa madalali na wachimbaji wadogo kukutana migodini kwani wanategemeana.

Mughanja alisema kwa miaka mingi wananchi wa mji mdogo wa Mirerani, wachimbaji wadogo wa madini hayo na madalali waliishi kwa kutegemeana hivyo ukuta huo usije kuwatenganisha.

Alisema wadau wote wanaouzunguka ukuta huo wanatarajia kunufaika kama miaka iliyopita hivyo wataendelea kutoa ushirikiano kama miaka iliyopita ikiwemo kulipa kodi ya serikali.




Mchimbaji mdogo wa madini ya Tanzanite Amos Andrew alisema ukuta huo unapaswa kuchochea maendeleo ya wachimbaji hao na siyo kuwadhoofisha.

Andrew alisema wachimbaji wa madini wanatambua kuwa ukuta huo una lengo la kudhibiti utoroshwaji wa madini ya Tanzanite hivyo hawaipingi serikali ila nao wanapaswa kusikilizwa.

Alisema pamoja na hayo, alitarajia kungekuwa na lango lingine kwenye eneo la Kilimanjaro mine ili wenye migodi ya pembezoni waweze kuingia kwa urahisi tofauti na sasa kwani ukuta huo una lango moja pekee.

Mwenyekiti wa chama cha wachimbaji wa madini Mkoani Manyara (Marema) Sadiki Mneney alisema wachimbaji madini wanapaswa kupewa ushirikiano wa kutosha juu ya ukuta huo.

Mneney alisema wachimbaji wadogo wameshatambua umuhimu wa kulipa kodi kwani walishakaa kikao na viongozi wa serikali na kuazimia kufungua ukurasa mpya na kuachana na yote yaliyopita.

No comments:

Post a Comment