Saturday 10 February 2018

RC MNYETI AWAFAGILIA MOFUGA NA KAMOGA

 MKUU wa Mkoa wa Manyara, Alexander Pastory Mnyeti amewapongeza Mkuu wa Wilaya ya Mbulu, Chelestino Mofuga na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya hiyo, Hudson Kamoga kwa kutimiza wajibu wao ipasavyo wakati wanapowatumikia wananchi wa eneo hilo.

Mnyeti akizungumza kwenye majumuisho ya ziara yake ya siku tano ya kutembelea halmashauri ya wilaya hiyo, alisema viongozi hao wanastahili pongezi kutokana na utendaji kazi bora wao kwa jamii.

 Alisema tangu akiwa mkuu wa wilaya ya Arumeru mkoani Arusha kabla ya kuteuliwa na Rais John Magufuli kuwa mkuu wa Mkoa wa Manyara, alikuwa anawasiliana na Mofuga kutokana na utendaji kazi bora anaoufanya.

"Mheshimiwa mkuu wa wilaya kupitia nafasi hii nakupongeza kwa dhati kutokana na utendaji kazi wako, nakutakia kila la heri ili siku moja upande cheo uwe mkuu wa mkoa," alisema Mnyeti.

 Alisema Mofuga ni kiongozi mwadilifu mwenye kuwatumikia wananchi wa Mbulu hivyo viongozi na wananchi wa wilaya hiyo wanapaswa kumpa ushirikiano wa kutosha.

“Ukiona kiongozi anabishana na mkuu wa wilaya basi huyo atakuwa na matatizo, wewe mkuu wa wilaya chapa kazi kwani hakuna mtu mwenye mapembe au sharubu kwenye wilaya hii ya Mbulu zaidi yako wewe Mofuga,” alisema Mnyeti.
 Alisema Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu, Hudson Kamoga ni kiongozi mchapakazi anayetekeleza wajibu wake ipasavyo na miaka ijayo atapandishwa cheo na Rais John Magufuli.

“Mkurugenzi wewe chapa kazi, Rais anavyombo vyake vingi vya uchunguzi atakuona tuu hata kama hayupo hapa kuna watu wake wanaandika andika na kufikisha taarifa ipo siku atakuona zaidi na kukupandisha cheo,” alisema Mnyeti.
 Alisema Kamoga japokuwa ana muda mchache tangu ateuliwe na Rais Magufuli kushikilia nafasi hiyo ametimiza wajibu wake ipasavyo kwa kuwatembelea wananchi na kusikiliza matatizo yao huku akisimamia vyema miradi ya maendeleo.

“Sina shaka na uadilifu wako kwani unafanya kazi kwa uadilifu umeanza vizuri wewe chapa kazi, mimi nilikuwa mkuu wa wilaya na leo ni mkuu wa mkoa kutokana na kufanya kazi hivyo fanya kazi utapanda cheo tuu,” alisema Mnyeti.
 Alisema ameanza kazi yake ya ukurugenzi wa halmashauri vizuri hivyo aendelee hivyo hivyo kwa kuwasimamia wakuu wa idara ili kuhakikisha wananchi wananufaika kwa kuwafanyia kazi.
 Hata hivyo, aliwataka viongozi hao kuhakikisha wanatekeleza maelekozo na maagizo yote alioyatoa kwenye ziara hiyo kwa kadiri muda alioupanga ili kuhakikisha wananchi wanapata majawabu ya changamoto na matatizo waliyotoa kwa wakati muafaka.

No comments:

Post a Comment