Saturday 10 February 2018

VIGOGO WA MADINI YA TANZANITE WATIWA MBARONI


Rais wa shirikisho la vyama vya madini nchini (Femata) John Bina akizungumza na wachimbaji madini ya Tanzanite wa Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara.

 Wachimbaji madini ya Tanzanite watiwa mbaroni 

Idadi ya vigogo wa madini ya Tanzanite waliokamatwa kwa amri ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Alexander Mnyeti, imeongezeka baada ya wengine wawili kukamatwa hivyo kufikisha idadi ya wachimbaji saba wa madini ya Tanzanite wa Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro na jijini Arusha, kushikiliwa na polisi wakidai kudhamini uchimbaji haramu wa madini hayo.


Awali, Mnyeti aliagiza vigogo hao watano wa madini hayo kukamatwa na kushikiliwa kwenye kituo cha polisi Mirerani ila wameongezeka wengine wawili na kufikia saba wakidaiwa kufadhili uchimbaji huo haramu. 

Akizungumza juu ya hilo, Kamanda wa polisi wa Mkoa wa Manyara, Agostino Senga alithibitisha kukamatwa kwa vigogo hao na kulazwa kituo cha polisi Mirerani.

Kamanda Senga alisema wanawashikilia baada ya kamati iliyoundwa na mkuu wa mkoa huo kupata taarifa kuwa vigogo hao wanashiriki kuwadhamini vijana wanaoingia kwa wizi kwenye migodi ya kampuni ya TanzaniteOne yenye ubia na serikali kwa asilimia 50 kwa 50 na shirika la madini la Taifa (Stamico).

Alisema bado wanaendelea na wanachunguza suala hilo na endapo utakamilika vigogo hao (majina yao tunayahifadhi) watafikishwa mahakamani.

"Bado tunaendelea na uchunguzi wa tukio hilo kwani watuhumiwa hao wanadaiwa kuwadhamini wachimbaji hao haramu ambao wanaingia migodini bila halali," alisema Senga.

Alisema kuna kamati maalum iliundwa na mkuu wa mkoa huo kwa ajili ya kuchunguza suala hilo hivyo baada ya uchunguzi wa awali, ikabidi vigogo hao wakamatwe.

Hata hivyo, Mwenyekiti wa chama cha wachimbaji madini wa mkoa wa Manyara (Marema) Sadiki Mneney alisema wamepata taarifa za kukamatwa na kushikiliwa polisi kwa wachimbaji hao.

Mneney alisema wao kama Marema wamepanga kwenye makao makuu ya mkoa huo mjini Babati kwa lengo la kuzungumza na mkuu wa mkoa huo juu ya kukamatwa kwa wachimbaji hao.

"Jumatatu ijayo tunaenda Babati kufuatilia suala hilo kwani hadi sasa hatujui ni sababu gani iliyofanya wachimbaji hao wa madini wakakamatwa na kushikiliwa na polisi," alisema. 

No comments:

Post a Comment