Thursday 8 February 2018

UWT SIMANJIRO YATOA MSAADA KWA WATOTO YATIMA MIRERANI



Wanachama wa Jumuiya ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) wa Chama Cha Mapinduzi CCM, Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara, katika kusherehekea miaka 41 ya kuzaliwa CCM, wametoa msaada wa vyakula kwenye kituo cha kulea watoto yatima cha Light in Africa cha Mji mdogo wa Mirerani na kupanda miti 20 kwenye taasisi za jamii.

Mwenyekiti wa UWT Wilayani Simanjiro, Naitapwaki Lemeya Tukai, akiongoza zoezi hilo kwa wanawake wa Kata za Endiamtu, Naisinyai na Mirerani, alisema jamii inapaswa kuwajali yatima na wanyonge.

Tukai alisema watanzania ni jamii ya watu wanaopendana hivyo, watoto hao wanapaswa kuangaliwa kwa hali na mali ili wasihisi upweke wa kuwakosa wazazi wanapaswa kuangaliwa kwa jicho la tatu kwani hao ni wanyonge.

Alisema ili kuwajali wanyonge kuanzia mwezi ujao wa Machi, yeye binafsi anajitolea sh50,000 kwa ajili ya kuongeza mishahara ya wafanyakazi watatu wa kituo hicho wanaowahudumia watoto hao.



Mlezi wa watoto hao wa kituo cha New Light, Eliese Munuo amewashukuru wanawake hao waliojitolea msaada huo kwa manufaa ya watoto hao wanyonge na yatima.

Munuo alisema kituo hicho cha Light in Africa kilichopo Mirerani, kinahudumia watoto wanyonge na yatima 69 wakiwemo wavulana 25 na wasichana 44.




Mjumbe wa Mkutano mkuu wa UWT ngazi ya Taifa, Jackline Momo alisema kila mmoja kwa nafasi yake binafsi anapaswa kutoa msaada kwa wahitaji hasa watoto yatima na wanyonge.

Momo alisema inampasa kila mmoja kwa wakati wake kurudi mwenyewe na kuangalia namna ya kuwasaidia watoto hao wanyonge, kwani nao wanahitaji upendo na misaada mingine kama watoto wenye kulelewa na baba na mama.

Katibu wa UWT wilaya ya Simanjiro, Zariha Mwinyi alisema wamepanda miti 10 kata ya Mirerani na miti 10 kwenye kata ya Endiamtu na kutoa zawadi ya mchele, unga, sabuni, sukari, mayai na juisi, kwa wanyonge kwenye kituo cha Light in Africa.

Mwinyi alisema pia katika maadhimisho hayo wamepokea wanachama wapya 40 wa CCM, wengi wao wakiwa wanafunzi wa shule za sekondari na wajasiriamali.

Diwani wa Tarafa ya Moipo, Paulina Makeseni alipongeza maadhimisho hayo kwa wanawake wa UWT wa kata tatu za Naisinyai, Mirerani na Endiamtu, kushiriki pamoja kwa nguvu moja kwa kutembelea yatima na wanyonge.

"Tunashukuru kupitia ngazi ya wilaya, tarafa na kata tumeshiriki pamoja maadhimisho haya, tunaiomba serikali iwape misaada watoto yatima na wanyonge, kupitia elimu na matibabu," alisema Makeseni.

No comments:

Post a Comment