Saturday 17 February 2018

DIWANI WA CHADEMA ALIYEJIUZULU AKANA KUNUNULIWA



 Diwani wa Kata ya Hayderer Wilayani Mbulu Mkoani Manyara, Justin Masuja (Chadema) ambaye amejiuzulu nafasi hiyo, kwa kujitoa kwenye chama hicho na kujiunga na CCM amesema hajanunuliwa ili kuondoka kwenye chama hicho.

Masuja ambaye ni diwani wa pili wa Chadema Mkoani Manyara, kujiuzulu kwenye kipindi cha wiki moja, baada ya diwani wa kata ya Bagara Mjini Babati, Nicodemus Tlaghasi kujiuzulu, amesema ameondoka Chadema kwa utashi wake mwenyewe. 

Alisema hata alipokuwa Chadema aliingia kwenye chama hicho kwa hiyari na utashi wake, hivyo hata CCM amejiunga nayo kwa ridhaa yake. 

"Wakati najiunga na Chadema nilikuja kwa ridhaa yangu hivyo hata kuhamia CCM nimefanya hivyo mwenyewe kwa haiba na utashi wangu," alisema Masuja. 

Alisema anapenda kuunga mkono harakati za Rais John Magufuli la kupambana na upigaji, rushwa na kuwatumikia wananchi hasa wanyonge ndiyo sababu akajiunga na CCM. 

Alisema akiwa Chadema hakuna mtu aliyempeleka hivyo amemtumia haki yake ya msingi kujiunga na CCM hivyo amehamia huko ili kufanikisha maendeleo ya wananchi wa eneo hilo. 

"Nawaomba CCM wanipokee kwa moyo mmoja kwani nilikuwa natekeleza ilani ya CCM nikiwa Chadema hivyo nimekuja kwenye chama hicho tukawatumikie wananchi ipasavyo," alisema Masuja. 

Hata hivyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu, Hudson Kamoga alithibitisha kupokea nakala ya barua ya kujiuzulu kwa diwani huyo. 

Kamoga alisema yeye kama msimamizi wa uchaguzi wa wilaya hiyo, atakijulisha chama alichotoka diwani huyo kuwa kata hiyo ipo wazi kwa sasa. 

Alisema pia wataiandikia barua tume ya Taifa ya uchaguzi ili mchakato wa uchaguzi mdogo wa udiwani kwenye kata hiyo uanze mara moja. 

No comments:

Post a Comment