Thursday 8 February 2018

RC MNYETI AWATAKA WATUMISHI MANYARA KUIUNGA MKONO SERIKALI



Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Alexander Mnyeti amewataka watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu, ambao hawaungi mkono Serikali inayoongozwa na CCM kuachia nafasi zao kwani atawachukulia hatua kali kwa kutotimiza wajibu wao ipasavyo kwa kufanya kazi kizembe na kuingiza siasa chafu kazini.

Kutokana na hali hiyo alimuagiza kaimu katibu Tawala wa mkoa huo Arnold Msuya kumsimamisha kazi ofisa Tarafa ya Dongobesh Bayo Banka hadi hapo atakapotoa maelezo ya kushindwa kutimiza wajibu wake kwa kuchanganya siasa na kazi.

Mnyeti alitoa agizo hilo wakati akizungumza na watumishi wa halmashauri ya wilaya ya Mbulu kwenye ziara yake ya siku saba.

Alisema CCM ilifanyika kampeni na kuinadi ilani yake kwa wananchi na kushinda uchaguzi kisha wakawakabidhi watumishi wawatumikie wananchi huku wakipewa mishahara na posho lakini wanashindwa kutekeleza kwa vitendo.

"Mnakaa ofisini na kulipwa mishahara na posho nyingi lakini mnashindwa kuwatumikia wananchi badala yake mnaingiza siasa chafu, natoa onyo kwa wote wasirudie jambo hilo hata mara moja nitawachukulia hatua kali," alisema Mnyeti.

Mnyeti alisema anayo majina na taarifa za baadhi ya watumishi wanafanya kazi kilegelege na kuzorotesha shughuli za serikali kwa kuingiza siasa kwenye kazi zao na kumkabidhi Msuya majina hayo.

"Pamoja na ofisa tarafa huyo pia nakukabidhi majina mengine ya watumishi ambao wanatekeleza maagizo ya viongozi wa vyama vingine vya kisasa badala ya kutekeleza maagizo ya viongozi wa serikali inayoongozwa na CCM," alisema Mnyeti.




Akisoma taarifa ya Wilaya ya Mbulu, Mkuu wa Wilaya hiyo Chelestino Mofuga alisema wilaya hiyo yenye halmashauri mbili ni miongoni mwa wilaya tano za mkoa huo.

Mofuga alisema wananchi wa eneo hilo ni wafugaji na wakulima, wenye kufanya shughuli zao katika maeneo tofauti kupitia halmashauri mbili za wilaya zilizopo Mbulu.

Alisema wilaya hiyo ina migogoro mbalimbali ya mipaka ikiwemo na Wilaya jirani za Hanang' Babati, Karatu Mkoani Arusha na Mkalama Mkoani Singida.

Alisema wamefanikiwa kutatua migogoro mingi ya ardhi wilayani humo kwani kila siku ya alhamisi akishirikiana na kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya na baadhi ya wakuu wa idara hukutana na wananchi wenye matatizo mbalimbali.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu, Hudson Kamoga alisema watumishi wa Halmashauri hiyo wamejipanga kuhakikisha wanawatumikia wananchi ipasavyo.

Kamoga alisema watumishi wa Halmashauri hiyo wapo tayari kutekeleza maagizo, maelekezo na ushauri katika kuwatumikia wananchi.

No comments:

Post a Comment