Thursday 8 March 2018

UMBULLAH NA MAHAWE WASAIDIA YATIMA MANYARA

 Katika kusherehekea wiki ya siku ya wanawake duniani, wabunge wa viti maalum wa Mkoa wa Manyara kwa tiketi ya CCM, Martha Umbullah na Ester Mahawe, wametoa msaada wa sare za shule na vifaa vya kuandikia kwa watoto yatima 43 wa shule ya msingi Bonga ya Mjini Babati.

Ester Mahawe akizungumza wakati wanakabidhi msaada huo wa sare za shule ikiwemo kaptula, mashati, sketi, blauzi, masweta, viatu, maboksi mawili ya kalamu, madaftari na majaladio, alisema umewagharimu sh1.6 milioni.

Mahawe alisema wametoa msaada kwa yatima hao kwani jambo lililo bora hapa duniani ni kusaidia wahitaji ndiyo sababu na wao wabunge wawili wakashirikiana kufanya hivyo.

"Ibada nzuri ni kusaidia wahitaji hata sisi wakristo na waislamu tunaambiwa kuwa tuwe tunawasaidia wenzetu na ndivyo tulivyofanya," alisema Mahawe.

 Mwalimu mkuu wa shule hiyo Januari Barnabas alisema kati ya wanafunzi hao yatima 43 wakiwemo wavulana 19 na wasichana 24.

Barnabas alisema wanakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo wanafunzi kutokula chakula cha mchana kwani nusu ya wanafunzi wa shule hiyo wanakaa umbali wa zaidi ya kilometa mbili.

Alisema pia wanakabiliwa na changamoto ya madarasa kwani yapo madarasa 15 na nyumba za walimu ni chache kwani wapo 22 na nyumba zilizopo ni tano zilizochakaa.


Hata hivyo, Martha Umbullah alisema changamoto ya wanafunzi kutokula shuleni inatakiwa ipatiwe ufumbuzi kwa kuwekewa mikakati kwani siyo jambo zuri wanafunzi kurudi nyumbani mchana kwa ajili ya kula.

Umbullah alisema viongozi wa eneo hilo akiwemo diwani na kamati ya shule wanapaswa kukaa pamoja na wazazi ili kufanikisha wanafunzi wapate chakula cha mchana shuleni.

"Japokuwa sisi siyo wabunge wa jimbo hili, lakini ni wabunge wa viti maalum wa mkoa tunafanya kazi kwenye wilaya zote tano na halmashauri saba zilizopo," alisema Umbullah.

Pia, msafara wa wabunge hao ulioongozana na Mwenyekiti na katibu wa UWT wa mkoa huo, Venosa Mjema na Haynes Munisi, ulitoa msaada wa vyakula kwa wanafunzi wa shule hiyo.

Msafara huo ulitoa magunia 12 ya mahindi, madebe 13 na nusu ya maharage, lita 60 za mafuta ya kupikia na mwanafunzi mmoja wa darasa la pili kushonewa sare hadi ahitimu darasa la saba.

No comments:

Post a Comment