Thursday 8 March 2018

MNYETI AWASHUKIA TARURA

Mkuu wa Mkoa wa Manyara Alexander Mnyeti ameagiza wakala wa barabara za mijini na vijijini (Tarura), kuwashirikisha viongozi wa maeneo husika pindi wanapotaka kuandaa bajeti za barabara ili kutosababisha migongano ya kutotambulika barabara zinazopaswa kupewa kipaumbele kwenye ukarabati na ujenzi.

Akizungumza jana mjini Babati kwenye kikao cha bodi ya barabara ya Mkoa huo, Mnyeti alisema Tarura ni chombo cha serikali hivyo wanatakiwa wawashirikishe viongozi wa maeneo husika ili kusiwepo na migongano tofauti na sasa kwani wanajitenga.


Mnyeti alisema Tarura wasijigeuze kuwa taasisi ya kipekee iliyopo serikali kuu ambayo haiwajibiki wilayani au mkoani ili hali ni wajibu wao kutoa taarifa na kushiriki vikao.

"Hizo barabara siyo za kwenu, sitaki kusikia mnapitisha barabara zijengwe ili hali viongozi wa wilaya hawajui au mimi sijui, ninyi Tarura msigeuze taasisi kuwa ya kwenu," alisema Mnyeti.

Alisema kwenye mkoa wake hataki ubabaishaji hivyo atamchukulia hatua kali meneja yeyote wa Tarura ambaye anafanya kazi kwa mazoezi badala ya kushirikisha viongozi wa maeneo husika.

Meneja wa wakala wa barabara nchini (Tanroads) mkoani Manyara, mhandisi Bashiri Rwesingisa alisema wanasimamia mtandao wa barabara wenye urefu wa kilometa 1,656 na madaraja 217, kati ya hizo kilometa 206 ni barabara kuu na kilometa 1,449 ni barabara za mkoa.

Mhandisi Rwesingisa alisema kilometa 206 za barabara kuu ni za lami kufuatia kukamilika kwa kipande cha Bereko- Bonga kwenye barabara ya Dodoma-Babati.

Alisema kwa upande wa kilometa 1,449 za barabara za mkoa, kilometa 40 ni za lami na kilometa 1,409 ni za changarawe.

"Hali ya barabara ni ya kuridhisha ingawa kuna baadhi zinapitika kwa shida wakati wa mvua hususani zilizopandishwa daraja mwaka 2009 kutoka kuwa za wilaya hadi kuwa za mkoa," alisema mhandisi Rwesingisa.

Alitaja baadhi ya barabara zilizoathirika na mvua zilizonyesha hivi karibuni ni Mbuyu wa Mjerumani-Mbulu, Kibaya-Dosidosi, Kilimapunda-Kidarafa, Losinyai-Njoro, Mogitu-Haydom na Singe-Kimotorok-Sukuro.

Meneja wa Tarura wilaya ya Simanjiro, mhandisi Martin Mwashambwa alisema wilaya hiyo ina mtandao wa barabara upatao kilometa 1,373.68


Mhandisi Mwashambwa alisema barabara za wilaya ni kilometa 932. 58 barabara za vijiji kilometa 327.96 na barabara za miji ni kilometa 137.14.

No comments:

Post a Comment