Saturday 12 April 2014

POLISI JAMII



Ofisa Polisi Jamii wa Tarafa ya Moipo Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara, Mkaguzi Msaidizi wa Polisi, Amiri Mlemba, akizungumza mwishoni mwa wiki na wakazi wa Kitongoji cha Kilimahewa Kata ya Endiamtu kuhusiana na suala zima la polisi jamii na ulinzi shirikishi.



Jamii Nchini imetakiwa kutoa ushirikiano kwenye suala zima la ulinzi shirikishi na polisi jamii ili kufanikisha ulinzi na usalama katika maeneo wanayoishi na kutokomeza ualifu. 

Wito huo umetolewa na Ofisa polisi jamii wa Tarafa ya Moipo Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, Mkaguzi Msaidizi wa polisi Amiri Mlemba wakati akizungumza na wakazi wa Kitongoji cha Kilimahewa Kata ya Endiamtu.

Mlemba alisema jamii ikitoa ushirikiano kwa polisi kupitia dhana ya ulinzi shirikishi na polisi jamii, uhalifu nchini utapungua na pia wananchi wataishi kwa amani ya kutosha na kufanya kazi zao za uzalishaji mali bila tatizo lolote.

“Kama mnavyotambua sisi polisi hatuwezi kufahamu kila jambo na pia wahalifu mnaishi nao mitaani hivyo kupitia dhana ya polisi jamii na ulinzi shirikishi tujulisheni wahalifu walipo au sehemu uhalifu unapofanyika ili tuutokomeze,” alisema Mlemba.



Hata hivyo, aliwataka wakazi hao kutokuwa na hofu pindi wanapotoa taarifa kwao na endapo watakuwa na wasiwasi watoe taarifa za uhalifu kwake au kwa mkuu wa kituo cha polisi Mirerani, SP Ally Mohamed Mkalipa. 

Kwa upande wao, wakazi hao walitoa pongezi kwa askari wa kituo hicho kwa kuwapa ushirikiano pindi wanapopewa taarifa za uhalifu, hivyo kusababisha ualifu kupungua kwenye mji mdogo wa Mirerani.

Walidai kuwa japokuwa askari polisi wanakabiliwa na tatizo la ukosefu wa nyumba za kuishi hivyo wanapopewa taarifa hutoka nyumbani na kwenda kituo cha polisi kisha kwenye tukio, lakini wanajitahidi kutimiza wajibu wao.

No comments:

Post a Comment