Wednesday 23 August 2017

NILIJIITA MJOMBA HUSSEIN ILI NIZAME KWENYE MIGODI YA TANZANITE-PILI HUSSEIN

 Pili Hussein ni mmoja katiya wanawake wachache wa Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, waliobahatika kuwa na mgodi wa madini ya Tanzanite.
 
Akiwa mmiliki wa mgodi huo, Pili alibahatika kupata madini ya Tanzanite na kufanikiwa kuwekeza kwenye miradi mbalimbali na kujenga nyumba, kununua magari, mashamba, matrekta na pikipiki.

Kuchimba madini ni kazi ngumu ya shuruba yenye kuhitaji mitulinga, yeye ni mwanamke alifanikiwa kwa namna ipi kuzamia mgodini na kufanya kazi hiyo bila kugundulika kuwa ni mwanamke.

Pili Hussein ambaye anaelezea changamoto alizozipata mara baada ya kufika kwa mara ya kwanza miaka ya 80 kwenye machimbo hayo ya Tanzanite
 
Mwandishi:Ilikuaje ulipofika kwa mara ya kwanza kwenye machimbo ya madini ya Tanzanite?

Pili: Wanawake walikuwa hawaruhusiwi kuzamia mgodini hivyo nikatamani kufanya shughuli hiyo ya kuchimba madini ili nipate fedha nyingi hivyo ilinibidi nibadili jina na kujiita mjomba Hussein kasha nikakata suruali zangu zikawa kaptula nikawa nazivaa na kuzamia mgodini.

Mwandishi: Baada ya hapo ikawaje?

Pili: Nilikuwa kama mwanaume kabisa kwani nilifunga panga kiunoni nikizamia mgodini umbali wa zaidi ya mita 100 chini ya ardhi kwenye vumbi, joto huku nikifanya kazi hiyo ngumu kama mwanaume halisi kumbe mimi ni mwanamke.

Mwandishi: Ulifanikiwa kupata madini ya Tanzanite ulipokuwa unachimba madini hayo?

Pili: Baada ya muda wa mwaka mmoja na miezi kadhaa nilipata utajiri wa madini hayo ya Tanzanite, kisha nikawajengea nyumba wazazi wangu mkoani Singida, ndugu zangu pia nikawajengea nyumba kisha nikaanzisha mgodi wangu binafsi ambao nao ulikuja kutoa madini nikanunua mashamba, magari, trekta, pikipiki na kujenga nyumba.
Mwandishi: Katika uchimbaji wako migodini, wachimbaji hawakuwahi kukuhisi kama wewe ni mwanamke?

Pili: Haikuwahi kutokea hivyo kwani hata sauti yangu ilikuwa ni kubwa ila siku moja ilitokea mwanamke alibakwa na watu kadhaa na polisi walipokuja kutukamata ndipo nikaeleza ukweli mtupu kwa kufika kituoni na kuwaomba askari wa kike wanikague kama nina uwezo wa kubaka na waliponiangalia ndipo wakabaini kuwa mimi ni mwanamke japo watu hawakuamini ila baadhi hawakuamini hadi nilipoolewa mwaka 1991 ndipo wakaamini.

Mwandishi:Kuna wanawake ambao wanazamia mgodini hadi hivi sasa?
Pili: Zaidi yangu mimi hakuna mwanamke ambaye anazamia mgodini kama mimi ila wapo wapishi migodini na ambao wanachekecha mchanga au udongo uliotoka mgodini ambao wanafanya shughuli hiyo juu mgodini ila hawaruhusiwi kuingia mgodini. 

Mwandishi: Unatoa wito gani kwa Serikali kuhusiana na kuwajengea uwezo wanawake wanaomiliki migodi, ambao wanachimba madini ya Tanzanite?

Pili: Serikali inapaswa kuwapa kipaumbele wanawake wanaomiliki migodi na kuchimba madini ya Tanzanite kwa kuwapatia mikopo kwani wengi wao wanakabiliwa na changamoto kubwa ya ukosefu wa fedha za uendeshaji wa shughuli za migodini hasa sisi ambao migodi yetu haijatoa madini kwa muda mrefu.

No comments:

Post a Comment