Monday 15 October 2012

UCHAGUZI CCM


Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoani Manyara kutoka wilaya ya Mbulu wakiteremka kwenye basi kwa ajili ya kuingia kwenye ukumbi wa CCM mjini Babati ili kuwachagua viongozi wa CCM wa mkoa huo.

Diwani wa Kata ya Loiborsiret Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara,Lucas Ole Mukusi amechaguliwa tena kuwa Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa mkoa huo kwa kipindi kingine cha miaka mitano.
Akitangaza matokeo ya uchaguzi huo uliofanyika juzi mjini Babati,Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar,Pandu Amiri Kificho alisema Ole Mukusi alishinda nafasi hiyo kwa kupata kura 629.
Kificho alisema wagombea wengine wawili waliopitishwa kugombea nafasi hiyo walijitoa lakini walipigiwa kura ambapo Godwin Nagol Kapurwa alipata kura 19 na Issa Omary Katuga alipata kura 18.
Alisema Fratey Massay alichaguliwa kuwa Katibu wa Siasa na Uenezi wa mkoa huo kwa kupata kura 41 na kuwabwaga wagombea wengine Michael Ngayda Tsaxara aliyepata kura 9 na Ernest Fiita Sulle alipata kura 2.
Alisema nafasi ya Katibu Uchumi na Fedha ya mkoa huo ilibidi irudiwe baada ya mshindi kutopata nusu ya kura kwani Lucas Zacharia alipata kura 26 Gidamon Gapchojiga kura 14,Janes Darabe kura 9 na Gabriel Bukhay kura 3.
Hata hivyo,uchaguzi huo uliporudiwa Kificho alimtangaza Diwani wa Kata ya Endiamtu,Zacharia kuwa Katibu Uchumi na Fedha wa mkoa wa Manyara kwa kupata kura 34 dhidi ya Gapchojiga aliyepata kura 18.


No comments:

Post a Comment