Saturday 21 June 2014

UKATILI WA MTOTO KITETO



Mtoto wa jamii ya kifugaji wa Kijiji cha Ndaleta, Wilayani Kiteto Mkoani Manyara, amepatwa na ugonjwa wa kichaa cha mbwa, baada ya kung’atwa na mbwa na daktari aliyemtibu kudaiwa kumpiga sindano ya kuzuia pepo punda badala ya kumpa tiba ya kung’atwa na mbwa.

Baba wa mtoto huyo, Loshiye Koronya, akizungumza kwenye hospitali ya wilaya ya Kiteto, baada ya madaktari kumuhakikishia kuwa mtoto wake Mgeno Koronya (3) hatapona, alielekeza malalamiko yake kwa daktari aliyempa dawa.

Koronya alisema daktari wa zahanati ya Njoro wilayani humo (jina tunalo) alimdai sh90,000 ambazo alimpatia ili amtibu mtoto wake, lakini badala ya kumpa tiba sahihi yeye akamchoma sindano ya kuzuia pepo punda.

Alisema mtoto wake aling’atwa na mbwa mwanzo mwa mwezi Mei mwaka huu, kisha akampeleka mtoto huyo kwenye zahanati hiyo ili apatiwe matibabu lakini Mei 15 Mgeno akazidiwa na kupata ugonjwa wa kichaa cha mbwa.

“Madaktari wamenihakikishia kuwa mwanangu hatapona na akiishi zaidi ya siku tatu nimshukuru Mungu, ila huu ni uzembe wa dokta Steve ambaye alichukua fedha zangu lakini hakumtibu ipasavyo mtoto wangu,” alisema Koronya.



Alisema baada ya Mgeno kupata ugonjwa wa kichaa cha mbwa, daktari huyo alidai kuwa huenda mbwa aliyemng’ata, naye aling’atwa na fisi kwani dawa alizompatia zingemaliza tatizo hilo lakini haikuwa hivyo. 

Hata hivyo, Kaimu mganga mkuu wa wilaya ya Kiteto, Dk Leadry Malisa alithibitisha Mgeno kupata kichaa cha mbwa, kwani dalili zote za kuogopa maji na kuwa na mate mengi mdomoni anazo, hivyo kupona kwake ni bahati.

“Inaonyesha virusi vimeshafika kichwani na kupona kwake ni kazi sana, huenda tatizo hili limesababishwa na kutohifadhiwa vizuri kwa sindano iliyotumika au dawa iliyotumika kumtibu siyo yenyewe,” alisema Dk Malisa.

Alisema atafuatilia suala hilo kwenye zahanati hiyo ya Njoro kwa kupata maelezo ya daktari huyo aliyempa huduma mtoto huyo, baada ya kung’atwa na mbwa, ili kubaini sababu iliyofanya hali hiyo imtokee Mgeno.

Kwa upande wao baadhi ya wakazi wa Kibaya waliomuona mtoto huyo akiwa hospitalini hapo walisikitishwa na kitendo hicho kwani kila wakati mtoto huyo alikuwa anapiga kelele na wakaiomba Serikali imchukulie hatua mganga huyo.

No comments:

Post a Comment