Saturday 21 June 2014

KWENYE TANZANITE HAKUNA MANYOKA



Utumikishwaji wa watoto wenye umri chini ya miaka 18 (nyoka) kwenye migodi ya madini ya Tanzanite, Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, hivi sasa haupo katika migodini hiyo, imeelezwa.

Hayo yalielezwa na Ofisa maendeleo ya jamii wa mji mdogo wa Mirerani, Isack Mgaya ambaye alidai kuwa alitembelea migodi 49 ya madini ya Tanzanite na kuzungumza na viongozi wa migodi hiyo juu ya kupiga vita ajira za watoto.

“Tulichunguza na kutembelea ili kuikagua migodi tofauti, ambapo tulikutana na mameneja na wamiliki wa migodi, ambao kwa kiasi kikubwa walituelewa na tuliwaeleza kuwa ni kinyume cha sheria kutumikisha watoto,” alisema Mgaya.

Alisema kuwa baada ya kuchunguza na kujiridhisha kuwa hakuna ajira ya watoto kwenye migodi hiyo ya Tanzanite, walitoa elimu kwa mameneja 19 juu ya utumikishwaji watoto na wakaunga mkono jitihada hizo kwa kutowaajiri.



Hata hivyo, Mwenyekiti wa chama cha wachimbaji wadogo wa madini mkoani Manyara, (Marema) Tawi la Mirerani, Japhary Matambi alikanusha vikali kutumika kwa watoto (nyoka) kwenye migodi ya madini ya Tanzanite.

“Hili jambo tumeshalipiga marufuku na tulishawaeleza wachimbaji wa madini ya Tanzanite kuwa mtu akikutwa anamtumikisha mtoto kwenye mgodi wake, atapigwa faini ya sh500,000 hivyo hilo jambo halipo huku,” alisema Matambi.

Miaka ya mwanzoni mwa mwaka 2000 kulikuwa na zaidi ya watoto 100 waliokuwa wanafanya kazi kwenye migodi hiyo, ila kutokana na jitihada za asasi ya Good hope chini ya mkurugenzi wake Dorah Mushi, ajira hizo zilisitishwa.

Kupitia Good hope watoto hao walikusanywa na wengine kurudishwa shule za msingi kusoma huku baadhi yao wakipelekwa kufundishwa ufundi mbalimbali ikiwemo wa useremala, magari, pikipiki na hadi sasa wanaendelea na kazi hizo.

No comments:

Post a Comment