Monday 22 December 2014

WAZEE WA KIMILA WAWAPONGEZA WANANCHI WALIOMSIMIKA KIONGOZI WALIOMCHAGUA


Wazee wa jamii ya kifugaji wa kimasai (Malaigwanan) wa Kata ya Naisinyai Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, wameunga mkono kitendo cha wananchi wa Kijiji cha Kambi ya Chokaa kumsimika Joshua Kuney kuwa Mwenyekiti wa Kijiji hicho.

Wakizungumza na waandishi wa habari, wazee hao walisema wananchi hao walichukua uamuzi sahihi wa kumsimika Kuney kwani alishinda kura ya maoni ya CCM kwa kupata kura 335 dhidi ya Mbuki Mollel aliyepata kura 215.

Desemba 14 mwaka huu, wananchi wa kijiji hicho walimsimika Kuney kuwa Mwenyekiti wa kijiji hicho baada ya uongozi wa CCM wilaya hiyo kukata jina lake na kumpitisha Mollel ambaye alishika nafasi ya pili.



Mmoja kati ya wazee hao Kisota Lengitambi (74) alisema malaigwanan wanaunga mkono uamuzi wa wananchi hao kwani wamemsimika mtu waliyemchagua wao na siyo chaguo la viongozi wa CCM wilaya hiyo.

“Nawapongeza wananchi kwani hawa viongozi walitaka kuleta vurugu na kuhatarisha amani kwenye kijiji cha Kambi ya Chokaa, kwani wananchi walimchagua mtu wanayempenda wao na siyo huyo Mollel chaguo la wilaya,” alisema Lengitambi.

Naye, Mwenyekiti wa CCM Kata ya Naisinyai Mosses Makeseni alisema kitendo cha wilaya kukata jina la mshindi na kumpitisha aliyeshindwa ni kudharau uamuzi wa wananchi wenye maamuzi sahihi na yenye busara.

“Walitaka kuhatarisha hali ya amani kwenye eneo hili ila wananchi walikuwa wavumilivu na kuchukua uamuzi wa busara, hivyo viongozi waliosababisha hali hiyo inatakiwa wachukuliwe hatua,” alisema Makeseni.

Alisema hawatambui huyo Mollel chaguo la wilaya anawaza kufanya jambo gani kwani yupo mafichoni na hajawahi kufika kwenye kijiji hicho tangu tukio hilo lifanyike na kuwapa wananchi wasiwasi wa kutotambua mustakabali huo.

Hata hivyo, Katibu wa CCM Mkoa wa Manyara, Ndengaso Ndekubali ambaye aliwaagiza viongozi wa CCM wilaya ya Simanjiro kumpitisha Kuney ambaye ni chaguo la wananchi na agizo hilo kutotekelezwa alisema atatoa uamuzi kuhusu hilo
hivi karibuni.

“Kama wananchi wameamua kufanya jambo hilo kwa kumsimika yeye kuwa kiongozi wao baada ya kumchagua nitatoa tamko la CCM mkoa hivi karibuni ili kuhakikisha suala hilo linakuwa katika hali nzuri zaidi,” alisema Ndekubali.

No comments:

Post a Comment