Friday 8 June 2018

MAMLAKA YA MJI MDOGO WA MIRERANI YAGAWA VIWANJA

 MAMLAKA ya Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, imetenga viwanja 500 kwa ajili ya kuwapatia waathirika wa mafuriko yaliyosababishwa na mvua zilizonyesha hivi karibuni ili wajenge nyumba na kuhama mabondeni.

Mwenyekiti wa Mamlaka ya Mji mdogo wa Mirerani, Adam Kobelo akizungumza jana alisema waliopatiwa viwanja hivyo wanapaswa kujenga makazi yao baada ya kipindi cha miezi sita hadi mwaka mmoja baada ya kukabidhiwa viwanja vyao.

Kobelo alisema hawataruhusu wale wote waliopatiwa viwanja hivyo kuviuza kwani lengo lao ni kuhakikisha waathirika wa mafuriko wanahama mabondeni na kujenga makazi mapya.

"Tuliona ni busara kuwapa waathirika wa mafuriko na pia baadhi ya watu waliokuwa wanapangisha kwenye nyumba hizo ili watu wale wale wasije wakapata tatizo lile lile kwa mwaka kesho," alisema Kobelo.


Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Uchumi, Ujenzi na Mazingira wa Mamlaka ya Mji mdogo wa Mirerani, Rajabu Msuya, alisema suala la kugawa viwanja kwa wahitaji haijawahi kutokea tangu mamlaka hiyo ianzishwe.

Msuya alisema wamepitia changamoto nyingi ikiwemo lawama wakati wa zoezi la ugawaji wa viwanja hivyo japo wenyewe hawana hofu kwani wanafanya kazi ya jamii ambayo halikwepeki kulalamikiwa.

"Niwapongeze wenyeviti wote kwa kuendesha vizuri zoezi hili vizuri kuanzia Mwenyekiti wa mamlaka Adam Kobelo, Mwenyekiti wa kamati yetu Joseph Masasi na ofisa mtendaji wa mamlaka Evans Mbogo walisimama vyema kwenye jambo hili," alisema Msuya.

Mwenyekiti wa mtaa wa Tunduru, Christopher Chengula alisema wametoa viwanja kwa wananchi wa maeneo yote yaliyoathirika na watu wenye uhitaji.

Chengula alisema wananchi wa vitongoji saba vya mji mdogo wa Mirerani, ambao wameathirika na mafuriko na watu wenye uhitaji maalum wamepatiwa viwanja vya kujenga makazi mapya.

Mmoja kati ya wakazi wa mji mdogo wa Mirerani, Jacklin Momo aliipongeza serikali kwa kufanikisha zoezi hilo la ugawaji wa viwanja kwa waathirika wa mafuriko na watu wengine wenye uhitaji.

Momo alisema waathirika waliokumbwa na mafuriko kwenye maeneo yote ya mji mdogo wa Mirerani wamepatiwa viwanja vipya hivyo serikali inapaswa kupongezwa kwa jambo hilo.


No comments:

Post a Comment