Friday 8 June 2018

VEO ASIMAMISHWA KAZI KWA KUFUJA FEDHA ZA MRADI WA MAENDELEO

 MKUU wa Mkoa wa Manyara, Alexander Mnyeti amemuagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Babati, Hamis Malinga kumsimamisha kazi ofisa mtendaji wa Kijiji cha Ayasanda anayetuhumiwa kufuja sh13 milioni fedha za michango ya wananchi ya mradi wa zahanati.

Mnyeti akizungumza kijijini hapo, amemuagiza Malinga kuandika barua kwa mkuu wa chuo hicho ili mtendaji huyo John Simon ambaye hivi sasa anasoma chuo cha uongozi Hombolo jijini Dodoma arudi Babati.

Mkuu huyo wa mkoa alitoa agizo hilo mara baada ya mmoja kati ya wakazi wa kijiji hicho John Lorry kulalamikia kufujwa kwa fedha za wananchi walizochanga ili kufanikisha mradi huo wa zahanati.


Lorry alisema wananchi wa eneo hilo walichanga fedha zao kwa ajili ya kuufanikisha ujenzi wa zahanati yao kutokana na kutembelea umbali mrefu kufuata huduma ya afya lakini wakakwamishwa na ufujaji wa fedha hizo.

"Tulitegemea huyo mtendaji wa kijiji achukuliwe hatua kali kwa kufuja fedha zetu lakini wanabebana tuu hapa kwani alikuja akapiga siasa bila kurudisha michango ya wananchi ya ujenzi wa zahanati," alisema Lorry.

Akijibu kuhusu hilo mkuu huyo wa mkoa aliagiza mtendaji huyo wa kijiji kurudishwa mara moja kwenye eneo hilo ili ajibu tuhuma hizo na endapo atashindwa kuzilipa fedha hizo sh13milioni afikishwe mahakamani.

"Watendaji kama hawa ndiyo wanasababaisha wananchi wasichangie miradi mingine ya maendeleo kwani wanahofia fedha zao kuliwa badala ya kupelekwa kwenye lengo husika kama alivyofanya huyo mtendaji," alisema Mnyeti.

Aliwaagiza maofisa watendaji wa vijiji na kata za mkoa huo kuhakikisha wanasimamia vyema michango ya wananchi kwani atawachukulia hatua kali wale wote watakaobainika kufuja fedha za maendeleo.

"Mtumishi yeyote atakayefuja fedha Manyara na kuomba uhamisho akahamia mkoa wowote iwe Mwanza au wapi tutaandika barua kule utumishi ili arudishwe Manyara kisha tutamfukuzia kazi hapa hapa Manyara hawezi kukwepa hilo," alisema Mnyeti.

Hata hivyo, Malinga aliahidi kutekeleza agizo hilo kwa kuhakikisha mtendaji huyo wa kijiji anarejeshwa kijijini hapo kwa ajili ya kujibu tuhuma hizo zinazomkabili.

Alisema awali, alimuagiza mkaguzi wa ndani wa halmashauri ya wilaya hiyo, kukagua hesabu za mradi huo na kusoma taarifa yake mbele ya mkutano mkuu wa kijiji ambapo mtendaji huyo alijitetea kuwa hakufuja fedha hizo.


No comments:

Post a Comment