Friday 8 June 2018

WAZIRI UMMY MWALIMU AMFAGILIA MBUNGE UMBULLAH

 WAZIRI wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amempongeza Mbunge wa viti maalum Mkoa wa Manyara, Martha Umbullah (CCM) kwa kuwa mdau mkubwa wa kuwawezesha wanawake wa mkoa huo kiuchumi, kwani ameacha alama isiyofutika kwa wanawake wa mkoa huo.

Waziri Mwalimu aliyazungumza mjini Mbulu Mkoani Manyara, kwenye maazimisho ya miaka 25 ya shirika lisilo la kiserikali linaloshughulikia utoaji wa mikopo midogo midogo na mafunzo ya ujasiriamali  kwa wanawake (WEDAC).
Waziri Mwalimu alisema anatambua mchango mkubwa unaotolewa na Mbunge Umbullah kwa jitihada zake ambazo ameendelea kuchukua kupitia shirika la WEDAC ambapo wanaunga mkono jitihada za serikali katika kuwawezesha wanawake kiuchumi.

"Hongera sana mh.Umbullah wewe ni jembe na mimi naomba niwaambie sisi bungeni tunamtegemea sana, tunamtumainia sana, ni mama anayejitambua mwenye uchungu kabisa wa maendeleo ya wanawake wa Manyara lakini na maendeleo ya wanawake wa Tanzania, kwa hivyo naamini na nyie mtaendelea kushirikiana na serikali katika kufikia utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya CCM,” alisema Waziri Ummy.
 Alisema serikali itaendelea  kuweka mazingira wezeshi kwa ajili ya kufikiwa  kwa usawa wa jinsia  uwezeshaji wa wanawake ikiwemo kwa wanawake wa vijijini na ndio maana wakati serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Magufuli ilipoingia madarakani ilifanya mambo makubwa mawili kwa upande wa wanawake kuanzisha majukwaa ya kiuchumi ya wanawake, ambapo kwa mkoa lipo, na kwa Mbulu nalo pia lipo la kuwezesha wanawake kiuchumi ambalo lilianzishwa na makamu wa raisi Mama Samia Suluhu Hasan.

Alisema yale majukwaa yatasaidia wanawake wajasiriamali kukutana na kuzungumzia changamoto mbalimbali zinazowakabili, hivyo jukwaa la kuwawezesha wanawake kiuchumi ndilo  jukwaa rasmi la kiserikali, hivyo wafanye uhamasishaji wa kuwaungunisha wanawake wote kujiunge kwenye jukwaa hilo.

"Lakini pia tutaendelea na jitihada za kusimamia na kuratibu  utekelezaji wa mfuko wa maendeleo ya wanawake ambao unatoa mikopo yenye masharti nafuu kwa ajili ya kuwawezesha wanawake wajasiriamali  wadogo ili kuanzisha na kuendeleza biashara, viwanda vidogo, kilimo na shughuli zingine za kiuchumi," alisema Waziri Ummy.

Aidha kupitia hilo Halmashauri zimetakiwa kuchangia asilimia 4  kupitia mapato yao ya ndani kwa ajili ya kuwakopesha wanawake, asilimia 4 vijana na  asilimia 2 kwa ajili ya kuchangia mahitaji ya watu wenye ulemavu.

"Nashukuru kwa kupeleka fedha kwenye vikundi vya wanawake  vyenye jumla. ya sh.mil.21, 700,000 kutoka halamshauri ya wilaya ya mbulu lakini pia halmashauri ya mji wa mbulu," alisema Waziri Mwalimu.

Mbunge wa viti maalum mkoani Manyara  Martha Umbullah (CCM) alimshukuru Waziri Ummy Mwalimu kwa kukubali kuwa mgeni rasmi katika hafla ya maadhimisho ya miaka 25 ya shirika linaloshughulikia utoaji wa mikopo kidogo kidogo na mafunzo  ya ujasiriamali  (WEDAC).

Alisema WEDAC ipo  katika  misingi  ya utekelezaji wa ilani ya uchaguzi wa CCM  mwaka 2005 wakati alipoomba ridhaa ya kuongoza wanawake wa mkoa huo, aliwaambia wanawake kuwa yeye ni mtaalam wa kuomba fedha  kwa wafadhili  kwa ajili ya kukopeshana na kuinua uchumi wa wanawake, waliokuwepo kwa wakati ule wanalijua hilo.

Umbullah alisema kupitia mikopo hiyo yeye ameweka alama ya kudumu kwa kuwa hata yeye asipokuea mbunge, taasisi hiyo itaendelea kuwanufaisha wanawake wa mkoa huo iwapo wataendelea kuwa waaminifu katika urejeshwaji wa mikopo hiyo.

"Waliokuwepo kipindi kile cha mwaka 2005 wakati wa kuomba ridhaa ya kuwa mbunge kwenye mkoa wangu, nilisema kuwa mimi niliwaambia akina mama kuwa mimi ni mtaalam kwa kuomba fedha  kwa wafadhili kwa hivyo nitawatafutia  fursa  kwa wafadhili ili akina mama waendelea kiuchumi," alisema Umbullah.

Alisema kuna wanawake walianza kukopeshwa kwa sh.200,000 tu, lakini hadi hivi sasa wamefikia kukopa sh.mil.5,000,000, na wameweza kupata mafanikio mbalimbali yaliyowawezesha kiuchumi katika nyanja mbalimbali za kuwakomboa katika umaskini.

No comments:

Post a Comment