Wednesday 22 November 2017

NAIBU WAZIRI WA MADINI LADSLAUS NYONGO AWATAKA WAUZA VIFAA VYA UJENZI WA UKUTA KUTOPANDISHA VIFAA BEI

 Naibu Waziri wa Madini Ladslaus Nyongo amewataka wauzaji wa vifaa vya ujenzi wa ukuta unaozunguka migodi ya madini ya Tanzanite wa Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, kutowauzia wanajeshi bei ghali vifaa vinavyojengea ukuta huo. 

Nyongo aliyasema hayo alipotembelea mji mdogo wa Mirerani wakati wa ukaguzi wa ujenzi wa ukuta na eneo litakalofanyika mnada wa madini ya Tanzanite. 

  
Alisema shughuli za ujenzi wa ukuta ni za kujitolea siyo za biashara ya kupata faida hivyo wafanyabiashara wasitake faida. 

Alisema wafanyabiashara wanapaswa kutumia fursa ya ujenzi wa ukuta huo kwa kufanya biashara na kupata faida kidogo kuliko kuweka tamaa ya kuuza vitu bei ghali. 


"Rais John Magufuli wakati anazindua barabara ya lami ya Kia-Mirerani Septemba 20 mwaka huu alitoa agizo la kujengwa kwa ukuta kwa lengo la kulinda rasilimali hii adimu hivyo wafanyabiashara wasijinufaishe," alisema Nyongo. 

Aliwapongeza askari wa jeshi la kujenga Taifa kupitia shirika la Suma JKT kwa namna wanavyofanya shughuli hiyo ya kujenga ukuta kutokana na kasi iliyopo. 

Alisema ana imani kazi hiyo itachukua muda wa miezi sita kama Rais Magufuli alivyoagiza na wao kama wizara wataendelea kutoa ushirikiano kwa jeshi hilo. 
Awali, mkuu wa wilaya ya Simanjiro mhandisi Zephania Chaula alisema askari hao wanakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo ya magari yanayobeba vifaa vya ujenzi kusimamishwa na askari polisi wa usalama barabarani wa mkoa wa Arusha, hivyo kuwachelewesha kwenye ujenzi. 

Mhandisi Chaula alisema ili kuhakikisha hilo alifanyiki tena wameamua kuweka karatasi maalumu kwenye magari yanayobeba vifaa vya ujenzi wa ukuta huo ili wasisumbuliwe tena. 

Alisema walitoa taarifa ngazi ya mkoa wa Manyara ili wakutane na mkoa wa Arusha, kwa lengo la kuzungumza na kumaliza changamoto za ujenzi huo. 




No comments:

Post a Comment