Wednesday 22 November 2017

LOWASSA AMNADI MGOMBEA UDIWANI MAKIBA NA KUKANUSHA KUTAKA KWENDA CCM

Waziri Mkuu mstaafu na mjumbe wa Baraza Kuu la Chadema, Edward Lowassa, amemshukia Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mrisho Gambo kuwa asitafute umaarufu wa kisiasa kwa kutumia jina lake. 

Akizungumza jana kwenye mkutano wa kampeni ya kumnadi Joyce Rutha (Chadema) mgombea udiwani wa kata ya Makiba Wilayani Arumeru Mkoani Arusha, Lowassa alisema hujatuma watu kwa Gambo ili arudi CCM. 

Alisema kuendelea kumzungumzia Gambo kwenye majukwa ya kisiasa ni kumpa umaarufu wa bure kwani yeye hujamtuma mtu au watu kutoka Monduli ili aende kwa mkuu huyo wa mkoa kwa lengo la kuomba arudi CCM. 


  
Mkuu wa mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo jana kwenye kurasa zake za mitandao ya kijamii ya Facebook, Instagram na tweeter, aliandika kuwa amepokea ujumbe kutoka Monduli. 

Gambo aliandika kuwa ujumbe huo ulikuwa na ombi moja kubwa amuombee mzee wa Monduli kwa Rais Magufuli ili akubali kumuona na yeye yupo tayari kurudi nyumbani kama Rais atakubali kumuona. 

Alisema ujumbe huo unasema ombi hilo katuma muda mrefu bila majibu. 

"Mnao mfahamu mzee huyu mfikishieni ujumbe kuwa salamu nitaifikisha,  mjumbe hauwawi," aliandika Gambo.

  
Lowassa alisema jana mchana alisoma kwenye mitandao ya kijamii kuwa ametuma watu wamuombee ili arudi CCM jambo ambalo siyo kweli. 

"Siwezi kumjibu huyu kijana kwani kuendelea kumjadili ni kumpa umaarufu hivyo simjibu chochote kwenye hilo," alisema Lowassa. 

Akizungumza wakati wa kumnadi mgombea udiwani huyo, Lowassa aliwataka wananchi wa kata ya Makiba kumpa kura nyingi za ndiyo Rutha ili awe diwani wao. 

"Mwaka 2015 nilikuja kuwaomba kura na mkanipa kwa wingi sasa endeleeni kuikataa CCM kwa kumpa kura mgombea wetu wa Chadema Rutho," alisema Lowassa. 

Pia, alisema wananchi zaidi ya milioni sita waliompigia kura nao wanapaswa kusemewa na wao kwa kuwepo kwa serikali ya mseto. 

Alisema katiba mpya ni jibu kwa kuweka kipengele cha serikali ya mseto kwa mlengo wa kushoto na kulia ili mtu mmoja asipate nafasi ya kuharibu vitu vingi. 

Alisema hata Marekani na Ufaransa wanashirikiana kwenye nafasi hizo pindi uchaguzi ukifanyika bila kujali chama ni cha kijamaa au kibepari. 

"Japo kuna wabunge lakini wale watu milioni sita walionipigia kura nao wanapaswa kuwakilishwa serikali kama wale milioni nane wengine ambao wana mawaziri, wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya, wakurugenzi na viongozi wengine," alisema Lowassa. 


 Mbunge wa jimbo la Arumeru mashariki Joshua Nassari alisema Makiba wanapaswa kumchaua Rutha kwani kuna Chadema inaendesha shughuli zake bila kujali ukabila ndiyo sababu tarafa hiyo ikapata Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Meru. 

Nassari alisema wananchi wanapaswa kumchagua Rutha bila kujali kabila lake kwani jambo la muhimu ni kusimamia maendeleo. 

Alisema Rutha ni mgombea mwadilifu kwani wapinzani wao waliweza kumrubuni kwa sh5 milioni na kumwekea pingamizi lakini tume ikamrudisha. 

"Kama hawamuogopi Rutha kwa nini wanamwekea vipingamizi wasije kwa debe, waje kwa debe tupambane wananchi waamue wenyewe, yule kijana aliuza utu wake kwa sh2 milioni lakini huyu sh5 milioni alizikataa," alisema Nassari. 
 Mbunge wa jimbo la Simanjiro James Ole Millya alisema ana imani kubwa na watu wa Makiba watampa kura nyingi Rutha ili awe diwani wao. 

Ole Millya alisema anashangazwa na watu waliokuwa Chadema kisha wanarudi CCM ili hali hakuna jambo kubwa walilofanyiwa hadi kusababisha kuachana na chama hicho zaidi ya tamaa. 

"Ni kwa furaha gani wewe Mollel unarudi CCM, ili hali wafugaji wanaendelea kuteseka kote Tanzania, jibu la yote hayo ni kuendelea kuwa Chadema na siyo kukimbia," alisema Ole Millya. 
 Mgombea udiwani wa kata hiyo Joyce Rutha alisema endapo atachaguliwa kuwa diwani, atahakikisha anakuwa mwakilishi mwema wa wananchi wa eneo hilo kwenye halmashauri ya wilaya hiyo. 


 Rutha alisema ataendelea kufanya kampeni ya nyumba kwa nyumba ili ahakikishe Chadema inashinda kwenye nafasi hiyo. 


No comments:

Post a Comment