Monday 1 August 2016

SIMANJIRO KUKABILIANA NA MIGOGORO YA ARDHI



Mkurugenzi Mtendaji mpya wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara, Yefred Myenzi amesema atahakikisha anakabiliana na migogoro ya ardhi kwa kusimamia sheria za ardhi na kuimarisha mabaraza ya ardhi ya vijiji na kata.

Myenzi akizungumza wakati akisoma salamu zake kwenye kikao cha robo ya nne cha baraza la madiwani wa halmashauri hiyo alisema atahakikisha mabaraza ya ardhi ya vijiji na kata yanaundwa kwenye sehemu ambapo hayapo.
Alisema karibu kila kijiji cha wilaya hiyo kina migogoro ya ardhi yenye sura nyingi ukiacha ile inayotokana na kukosa uelewa na baadhi ya maeneo ambayo migogoro yake inahusu uvamizi na kuibukua kwa soko holela la kuuza ardhi.



“Ipo migogoro yenye sura ya kisiasa na mingine ya kukosa uelewa ila migogoro mingi inachochewa na uhaba wa rasilimali hasa malisho na maji nyakati za kiangazi na nitapambana nayo ili tuhakikishe tunaimaliza,” alisema Myenzi.

Hata hivyo, alisema halmashauri hiyo ina malengo ya kupima viwanja 850 kwa mwaka ambayo atatoa msukumo wa kuhakikisha yanatimia ili kuepuka migogoro na kuwapa watu uhakika wa umiliki wa maeneo hayo


Alisema anaomba ushirikiano wa makundi yote ya kijamii hasa wafugaji na wakulima, mamlaka ya hifadhi, taasisi za umma na binafsi katika kupanga miji ya Orkesumet, Mirerani na maeneo mengine ya biashara yanayokua kwa kasi. 

Alisema moja ya dhamana kubwa aliyopewa kwa kazi yake ni kuhakikisha anasimamia upatikanaji wa halali, mgawanyo wa haki na matumizi sahihi ya rasilimali za umma ili kuwezesha upatikanaji huduma za msingi na maendeleo.



“Wenzetu waliotutangulia walifanya walichoweza kwa nafasi yao na sisi tumepewa fursa hii tuitumie kuandika historia kwa vizazi vijavyo ili tuache urathi usiofutika kwa maisha ya wananchi wa simanjiro,” alisema Myenzi.

Alisema yote hayo yatawezekana ili mradi kuwepo na msukumo wa pamoja baina ya uongozi na wananchi na utekelezaji wa masuala hayo katka ngazi ya halmashauri na yapo maagizo ya kitaifa ambayo hayana budi kutiliwa mkazo.



Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Jackson Sipitieck alisema japokuwa Myenzi bado hajamaliza hata mwezi mmoja tangu aanze kazi kwenye eneo hilo lakini kwa muda mfupi waliokuwa nao anaonyesha ataisaidia wilaya hiyo.

Sipitieck alisema ana imani na mkurugenzi huyo na kwa kushirikiana viongozi wa wilaya hiyo, madiwani na watumishi wa halmashauri, watampa ushirikiano mkubwa na wakutosha ili jamii ya eneo hilo iweze kupata huduma stahiki

No comments:

Post a Comment