Monday 15 August 2016

MNADA WA MADINI YA TANZANITE WAFANYIKA ARUSHA



Madini ya Tanzanite yenye thamani ya dola 4.3 milioni za Marekani sawa na sh7.4 bilioni yameuzwa kwenye mnada wa madini hayo uliofanyika kwa muda wa siku nne jijini Arusha, huku Serikali ikipata mrabaha wa sh378 milioni.

Katika mnada huo, kampuni ya TanzaniteOne na Shirika la madini (Stamico) waliongoza kwa kuuza madini ya dola milioni 3.3 sawa na sh7.3 bilioni na serikali ikapata mrabaha wa sh367 milioni na kampuni ya Franone iliuza dola laki 1 sawa na sh235 milioni na serikali ikapata mrabaha wa10 milioni.



Mkurugenzi wa uthaminishaji wa madini ya almasi na vito wa Wizara ya Nishati na Madini, Archard Kalugendo aliyasema hayo jijini Arusha, wakati Mkuu wa mkoa wa Manyara, Dk Joel Bendera akifunga mnada wa madini ya Tanzanite.

Kalugendo alisema wachimbaji na wanunuzi walioshiriki mnada huo ni makampuni 37 na wachimbaji watano walijitokeza ni TanzaniteOne na Stamico, Tanzanite Africa/J.S Magezi, Chusa Mining, Kurian Laizer na Franone Gems.

Alisema makampuni yanayonunua na kuuza madini ndani na nje ya nchi yalishiriki mnada huo wenye lengo la kuhakikisha bei ya madini ya Tanzanite ambayo ilikuwa imeshuka inapanda na kuweka ushindani kwa njia ya minada.



Mkuu wa mkoa wa Manyara Dk Joel Bendera alisema madini ya Tanzanite yanapatikana eneo moja la Mirerani wilayani Simanjiro kwa hapa duniani hivyo serikali itaendelea kudumisha ulinzi na usalama kwa wachimbaji wa madini.

Dk Bendera alisema kwa mnada huo bei ya Tanzanite itauzwa inavyostahili pia serikali ya wilaya ya Simanjiro itaweza kukusanya mapato yake ya kodi za huduma kwa urahisi zaidi na hivyo kutoa huduma za jamii kwa ufanisi zaidi.

“Natoa wito kwa wachimbaji wote wa madini ya Tanzanite kujitokeza zaidi kwenye mnada ujao kwani huu kati ya migodi zaidi ya 180 iliyopo Mirerani ni wachimbaji watano pekee walioshiki katika mnada huu,” alisema Dk Bendera.



Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini Profesa James Mdoe kupitia mnada huo mapato ya nchi yataongezeka kupitia madini ya Tanzanite na serikali itakusanya mapato yake kwa urahisi zaidi kwani mnada unafanyika eneo moja.

Profesa Mdoe alisema kwa sababu mnada huo ni wa mara ya kwanza zipo changamoto zilizojitokeza kwani ni muda mfupu wa maandalizi ulikuwepo, ila serikali itendelea kuboresha minada ijayo ili wanufaike na madini ya Tanzanite.

“Kwa njia hii ya mnada huu pia tunakabiliana na suala la utoroshaji wa madini ya Tanzanite kwenda nchi za jirani kwani wanunuzi watapata fursa ya kufika kununua wenyewe kuliko kutorosha,” alisema Profesa Mdoe.

No comments:

Post a Comment