Saturday 30 July 2016

KAYA ZA WILAYA YA BABATI VIJIJINI ZATAKIWA KUJIUNGA NA CHF ILIYOBORESHWA



Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Dk Joel Bendera amewaagiza viongozi wa halmashauri ya Wilaya ya Babati kuhakikisha hadi Desemba mwaka huu kaya 40,642 zinajiunga na mfuko wa afya ya jamii ulioboreshwa (CHF) hivyo kufikia asilimia 50 ya kaya za wilaya hiyo.

Dk Bendera ameyasema hayo mbele ya mkuu wa Wilaya hiyo Raymond Mushi, Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo Hamis Malinga, wakati akizungumza na wananchi wa Tarafa ya Goroa, alipotembelea kuhamasisha kaya kujiunga na mfuko huo. 




Dk Bendera amesema wilaya hiyo ina kaya 81,284 hivyo viongozi wa wilaya hiyo wahakikishe hadi mwezi Desemba wawe wamefanikisha nusu ya kaya zijiunge na mfuko huo.

Ameeleza kuwa suala la kupatiwa matibabu pindi mtu akiugua halina mjadala hivyo viongozi wa ngazi tofauti kwenye wilaya hiyo wanapaswa kufuatilia ili kaya hizo zijiunge na mfuko huo ambao una manufaa kwao.





Mkuu huyo wa Mkoa amesema viongozi wote wa eneo hilo wanapaswa kuhakikisha jamii inajiunga na mfuko huo kwani ni ukombozi wao kwenye sekta ya afya na siku wakistaafu wananchi watawakumbuka kwa kusababisha mabadiliko ya huduma hizo.

“Naibu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Hamis Kigwangalla alitoa agizo kwa mkoa wa Manyara kuhakikisha baada ya miezi sita ijayo tufikie asilimia 50 ya kaya zote kujiunga na CHF iliyoboreshwa,” ameeleza.



Malinga amesema kupitia timu waliyonayo kuanzia ngazi ya vijiji, kata na tarafa, watatimiza majukumu yao kwa kupeana mrejesho kila mwezi ili kutambua wamefikia hatua gani na wanatarajia hadi mwezi Desemba watafanikisha.




Meneja wa mfuko wa Taifa wa bima ya afya nchini (NHIF) mkoani Manyara, Isaya Shekifu amesema mpango wa CHF ulioboreshwa utawawezesha kila kaya ya watu sita baba, mama na watoto wanne ambao hawajafikisha miaka 18 kupata matibabu kwa gharama ya sh30,000 katika mwaka mzima.


Shekifu ameeleza kuwa bima ya afya ni muhimu kwa sababu siyo kila mtu anapopata ugonjwa ana uwezo wa kugharamia matibabu na nchi zilizoendelea zimefanikiwa kupunguza vifo visivyo na lazima kwa kuhakikisha watu wanajiunga na mfuko.


“Katika CHF ya zamani huduma za nje tu ndizo zilizotolewa, hii iliyoboreshwa huduma ya magonjwa ya nje, kulazwa, upasuaji na vipimo ikiwemo x- ray zinatolewa kwa wanachama waliojiunga bila kulipia,” amesema Shekifu.

No comments:

Post a Comment