Saturday 26 March 2016

RAISA WA FEMATA ATEMBELEA MIGODI YA TANZANITE


Rais wa shirikisho la vyama vya madini nchini (Femata) John Bina amesema migogoro mingi ya madini baina ya wachimbaji wadogo na wachimbaji wakubwa inasababishwa na sheria mbovu za madini zinazotumika hivi sasa.

Bina alidai kuwa sheria nyingi za madini ambazo ni mbovu zimenakiliwa kutoka nchini Uingereza, ambapo hakuna madini ya vito ya Tanzanite na kutumika hapa nchini hivyo kusababisha migogoro ya mara kwa mara ambayo haimaliziki.

Akizungumza kwenye machimbo ya madini ya Tanzanite ya mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, alisema inatakiwa sheria hizo kandamizi ziondolewe ili wachimbaji wadogo wafanye kazi zao bila kuonewa.

Alitaja miongoni mwa sheria zinazowakandamiza wachimbaji wadogo kuwa ni sheria ya kuchimba madini ya vito ya Tanzanite kwa njia ya wima ili hali jiolojia ya madini hayo yanataka yachimbwe kwa njia ya mshazari.

Alisema kutokana na madini hayo kuwa Tanzania pekee, ingetakiwa sheria, kanuni na taratibu za uchimbaji wa madini ya Tanzanite uwe wa kipekee, kuliko hivi sasa wanapochukua sheria za nje na kuendelea kuzitumia hapa nchini.
Mwenyekiti wa chama cha wachimbaji madini mkoani Manyara (Marema) Sadiki Mneney alisema japokuwa tume nyingi ziliundwa na serikali ili kuhakikisha migogoro hiyo inamalizia lakini hazikufanikiwa.

“Tume nyingi zimeundwa na kufika Mirerani ili kumaliza migogoro yetu na mchimbaji mkubwa ila zikashindwa kumaliza ikiwemo ya Brigedia Jenerali Robert Mboma, Mang’enya, Jaji Mark Bomani na wabunge 25,” alisema Mneney.

No comments:

Post a Comment