Tuesday 1 March 2016

NYUMBA ZAEZULIWA NA UPEPO



Zaidi ya nyumba 25 za Kata ya Msitu wa Tembo na Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, ikiwemo darasa la shule ya msingi Zaire zimeezuliwa mapaa baada ya kutokea upepo mkali.

Kwenye kata ya Msitu wa Tembo kijiji cha Magadini nyumba 17 ziliezuliwa mapaa na kata ya Mirerani na Endiamtu zaidi ya nyumba nane ziliezuliwa kutokana na upepo huo mkali uliotokea kwa nyakati tofauti.

Akizungumzia kuhusu tukio hilo, mkuu wa wilaya hiyo Mahmoud Kambona alisema zaidi ya nyumba hizo kuharibika, hakuna mtu aliyejeruhiwa wala kufariki dunia kutokana na tatizo hizo ila kaya kadhaa zimekosa makazi.

Kambona alisema baada ya tukio hilo alitembelea kwenye baadhi ya maeneo yaliyokumbwa na tatizo hilo na ameshamuagiza mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo Lucas Mweri kukarabati darasa hilo lililoezuliwa paa.

“Hata hivyo, nyumba nyingi zilizoezuliwa paa ni zile ambazo zimejengwa kwa kutumia matofali ya udongo na nimeiasa jamii kujenga nyumba zao kwa matofali ya udongo ili ziwe madhubuti kuepuka matatizo,” alisema Kambona.



Kwa upande wake, Mwenyekiti wa kitongoji cha Twiga Anthony Musiba alisema kwenye kitongoji chake ni zaidi ya nyumba tano zimepata dhoruba ya kuezuliwa mapaa kutokana na upepo huo ila nyingine zimebomoka ukuta.

“Kwa tathimini ya haraka ni nyumba tano zimeezuliwa mapaa ikiwemo ya mjane Farida Juma ambayo paa lake lilitolewa na upepo na kutupwa kwenye nguzo ya umeme, pia vitongoji vingine vimeathirika” alisema Musiba.

Akizungumza baada ya ajali hiyo, mjane huyo Farida Juma alisema hivi sasa wamehamia kwa mmoja kati ya majirani zao, ili kujisitiri baada ya nyumba yao kuezuliwa na paa hivyo waangaliwe kwa jicho la huruma zaidi kwa msaada.

“Tunaiomba serikali na wasamaria wema watusaidi kwani tuna wakati mgumu hivi sasa ukizingiatia sisi ni wajane baada ya mtu tuliyekuwa tunamtegemea mchimbaji madini marehemu Dotto Ruta na sasa hatuna mwingine,” alisema.

No comments:

Post a Comment