Tuesday 1 March 2016

WAZEE 500 WAPATIWA MSAADA WA TANI 100 ZA MAHINDI



Wazee 500 wakiwemo vikongwe100 wa Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, wamepatiwa msaada wa magunia 100 ya mahindi yaliyotolewa na Mkurugenzi wa kampuni ya TanzaniteOne Hussein Gonga.

Mwenyekiti wa Saidia wana jamii Tanzania (Sawata) Mohamed issa Mughanja akizungumza mbele ya mkuu wa wilaya hiyo Mahmoud Kambona alisema msaada huo umetolewa na Gonga kwa ajili ya wazee wa shirika la Mwasi.

Mughanja alisema zaidi ya kuwapatia msaada huo wa magunia 100 ya thamani ya sh7 milioni, Gonga pia amewafungulia bima ya afya ya jamii (CHF) wazee hao ili wapate matibabu pindi wakiugua mara baada ya wazee hao kuomba hayo.

“Aprili mwaka jana Sawata ilimwandikia barua Gonga ya kukutana na wazee wa Mirerani na kuona namna ya kuwasaidia na mwezi Octoba alikutana nao na aliwaahidi kuwapa chakula magunia 100 na kuwafungulia bima ya afya” alisema. 



Ofisa mwandamizi wa Sawata, Mohamed Shauri akisoma risala ya kwa mkuu wa wilaya hiyo, alisema asasi yao ilianzishwa mwaka 2009 kwa kuisaidia utekelezaji wa kilimo, visima na sera ikiwemo elimu, ushauri na kutafuta wahisani.

Shauri alisema Sawata imeomba ardhi maeneo ya vijiji vya Kilombero, Magadini na Ngage, ili kuwajengea uwezo wakulima wa kilimo hai cha mboga mboga na matunda kwa njia ya umwagiliaji na kupatiwa mikopo ya pembejeo siyo na riba.

“Hata hivyo, Sawata na makundi iliyonayo tunakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo vitendea kazi vya ofisi, wazee wetu wanachangamoto nyingi na ukosefu wa ardhi ya kilimo kwani mpango wetu ni kutumia kilimo hai,” alisema.



Kwa upande wake, mkuu wa wilaya hiyo Mahmoud Kambona aliwataka wawekezaji wengine wa eneo hilo kuiga kitendo cha Gonga kwa kuwasaidia watu wenye uhitaji ikiwemo wazee ambao wanahitaji msaada.

“Japokuwa madini ya Tanzanite yanapatikana kwenye wilaya yetu ya Simanjiro lakini watu wanaofaidi ni kutoka nje ya eneo hilo, hivyo wawekezaji wengine wanatakiwa kuiga mfano wa Gonga kwa kusaidia jamii,” alisema Kambona.


No comments:

Post a Comment