Saturday 5 March 2016

MGUTWA KUGAWA MICHE 1,500 KWENYE SHULE ZA MSINGI NA SEKONDARI



Shule ya sekondari Mgutwa ya Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, imeazimia kugawa miti 1,500 kwa shule za msingi na sekondari za mji mdogo wa Mirerani ili kupambana na majanga ya upepo na mmomonyoka wa ardhi.

Akizungumza na wageni waliotembelea shule hiyo, meneja wa shule hiyo Monica Mlemeta, alisema wao ni wana mazingira, hivyo wataendelea kupanda miti mingi zaidi japo eneo hilo waliloligeuza kuwa la kijani tofauti na awali.

Mlemeta alisema shule hiyo ina wanafunzi wa kidato cha kwanza hadi cha nne, ina lengo la kuanzisha kidato cha tano hadi cha sita, ili kuboresha elimu ya eneo hilo la Simanjiro pamoja na kuzidi kutunza mazingira kwa kupanda miti mingi.



Alisema shule hiyo mwaka 2014 na 2015 iliotesha miti 1,000 ya kivuli na 300 ya matunda ili kutunza mazingira hivyo wanataka na shule nyingine zioteshe miti kwa kasi kubwa kwa ajili ya kuondokana na hali ya ukame na jangwa.

“Tutahakikisha miti hiyo inagawiwa kwa uwiano sawa kwa kila shule ya sekondari na msingi inayozunguka mji mdogo wa Mirerani na tutafuatilia ukuaji wake kwa ukaribu ili kila mche umemea na siyo kufa,” alisema Mlemeta.



Mratibu wa asasi ya Community Education resources foundation, Godfrey Lema walioipatia shule ya Mgutwa miti hiyo 1,500 alisema lengo lao ni kuhakikisha wanatunza mazingira na kuondokana na ukame uliopo katika eneo hilo.

Alisema  kwa kushirikiana na asasi za Nick’s Eco safaris na Moivaro jitegemee family wamefanikisha hilo, japo ardhi ya eneo hilo ina mwamba na magadi, uongozi wa shule umelibadili kuwa la kijani, kwa kuendeleza utunzaji mazingira na kuwa mfano wa kuigwa.



“Wageni wetu Megan Allen kutoka Marekani na Juliane Friedrich wa Ujerumani, wamefurahia ukijani uliopo hapa na tutahakikisha tunaendelea kuiunga mkono shule hii, kwani imekuwa mfano bora wa utunzaji mazingira,” alisema Lema.

Alisema elimu ya mazingira inatakiwa kutolewa kwa sehemu kubwa ya jamii ya wananchi wa wilaya ya simanjiro, ili kuhakisha wanapanda miti kwa wingi kwani ndiyo vyanzo vya mvua na kupata kivuli, matunda na hewa safi.


No comments:

Post a Comment