Saturday 1 March 2014

MGOGORO YAEDA CHINI



Wafugaji wa jamii ya wairaq na wadatoga wa Bonde la Yaeda Chini, Wilayani Mbulu Mkoani Manyara, waliokuwa na mgogoro wa muda mrefu wa eneo la malisho, wamechagua watu 40 watakaosuluhisha ugomvi wao.

Watu hao 40 wamechaguliwa ili kutatua mgogoro huo, baada ya Mkuu wa wilaya hiyo, Anatory Choya kuagiza wafanye hivyo na akawapa muda wa wiki mbili wawe wamekutana na kusuluhishana na atawatembelea tena Machi 18.



Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu, Zacharia Paul Isaay alisema kupitia vikao hivyo mauaji, vurugu na migogoro ya mara kwa mara itamalizika na kufanya jamii ya eneo hilo kuishi kwa amani kama awali.

“Mnatakiwa muachane na vurugu hizi ambazo hazina sababu za msingi, ninyi mmekuwa kama ndugu hivi sasa, kwani kuna wairaq wamewaoa wadatoga na kati yenu hapa kuna wadatoga wamewaoa wairaq,”  alisema Isaay.

Mgogoro wa Bonde la Yaeda chini umekuwa ukitokea mara kwa mara na hadi hivi sasa mauaji ya watu wanne yameshatokea, ambapo hivi karibuni mfugaji wa jamii ya kiiraqw, Moshi Masabeda (47) aliuawa kwa kuchinjwa kama kuku.




Akizungumza na jamii hizo, Choya aliagiza ili kumaliza mgogoro huo, inatakiwa wajadili kukomesha mauaji yanayotokea eneo hilo, kupiga vita wizi wa mifugo na namna ya kupanga matumizi bora ya ardhi.

Pia, aliwaagiza wajadili tatizo la uhamiaji haramu lililopo eneo hilo kwani kuna baadhi ya watu wamekuwa wakiingia kwenye bonde hilo bila taarifa kwa kutofuata sheria, kanuni na taratibu, ikiwemo kukubaliwa na wana kijiji husika.

“Nawaagiza watendaji wa vijiji na kata wa bonde la Yaeda Chini, hakikisheni hakutokei machafuko tena kwani ninyi mnapokea mishahara, hivyo fanyeni kazi kwa jasho na kuchukua hatua siyo kusubiri watu wa wilayani,” alisema Choya.

No comments:

Post a Comment