Saturday 30 December 2017

KOMBA MWENYEKITI WA UVCCM MANYARA KUPAMBANIA ASILIMIA 5 ZA MIKOPO YA VIJANA

 Mwenyekiti wa Jumuiya ya Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Mkoa wa Manyara, Mosses Komba (kulia) akiwa na vijana wenzake wakichagua mahindi ya kuchoma walipofanya ziara ya siku moja ya kutembelea wilaya ya Mbulu. 
 Mwenyekiti wa Jumuiya ya Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Mkoa wa Manyara, Mosses Komba (wa pili kulia) akipokea bendera ya Chadema kutoka kwa aliyekuwa mjumbe wa kamati tendaji ya Chadema Wilaya ya Mbulu Stephano Geje wa mji mdogo wa Haydom ambaye yeye na wanachama wengine 10 walijiunga na CCM mjini Mbulu.

 Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Manyara, Mosses Komba (watatu kushoto) akikagua jengo la UVCCM Wilayani Mbulu jana, ambalo liliungua na kuteketezwa na moto Desemba 14 mwaka jana.
 Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Manyara, Mosses Komba (wapili kushoto) akikagua jengo la UVCCM Wilayani Mbulu jana, ambalo liliungua na kuteketezwa na moto Desemba 14 mwaka jana.
Mwenyekiti wa UVCCM Mkoani Manyara, Mosses Komba akizungumza kwenye kikao cha baraza la UVCCM Wilaya ya Mbulu katika ziara yake ya kutembelea wilaya hiyo.

MWENYEKITI wa Jumuiya ya Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) Mkoani Manyara, Mosses Komba  amesema ameanza mchakato wa kuhakikisha Halmashauri za Wilaya za Mkoa huo zinawapatia vijana mikopo kupitia asilimia 5 ya mapato ya ndani.

Komba aliyasema hayo mjini Mbulu wakati akizungumza kwenye kikao cha Baraza la UVCCM la wilaya ya Mbulu.

Alisema ameshatembelea baadhi ya halmashauri na kukutana na wakurugenzi watendaji hao ambao wamempa utaratibu wa namna ya vijana hao kupata mikopo.

Aliwataka vijana hao kujipanga kwenye hilo kwa kuanzisha vikundi ili mikopo itakapoanza kutolewa wawe wamejiandaa kupitia umoja wao kwa ajili ya kufanikisha suala hilo na kuagiza viongozi wa UVCCM wa wilaya hiyo kusimamia hilo.

"Nilipofika hapa Mbulu nilipita kwenye ofisi ya mkuu wa wilaya Chelestino Mofuga ili kuzungumza naye aweke msukumo kwenye hilo nikamkosa kwani yupo likizo, lakini nimeacha ujumbe juu ya hilo, hivyo vijana mtumie fursa hiyo," alisema Komba.

Katibu wa UVCCM wilayani Mbulu, Malkiori Pantaleo alisema jumuiya hiyo ina wanachama 15,477 kati yao wanaume ni 9,105 na wanawake ni 6,372.

Pantaleo alisema hivi sasa wana mradi mmoja wa jengo na wamefanikiwa kurejesha ekari 12 za shamba la UVCCM lililokuwa na mgogoro tangu mwaka 2012 kwenye tawi la Getesh kata ya Tumati.

Alisema wapo kwenye mchakato wa ujenzi wa jengo la UVCCM la wilaya hiyo lililoungua kwa moto Desemba 14 mwaka jana, ambalo lilikuwa linaingiza kipato kwenye jumuiya hiyo.

Mbunge wa jimbo la Mbulu mjini Paul Zacharia Isaay, amewataka vijana kupitia ilani ya CCM na kutangaza mazuri yaliyofanywa na chama hicho.

Isaay alisema vijana wakiwa wanajibu hoja kwenye vijiwe mitaani na katika mitandao itasaidia kuweka ukweli hadharani pindi wapinzani wakipotosha maendeleo yaliyofanyika.

Mbunge wa jimbo la Mbulu Vijijini Flatei Massay amewataka vijana wajitokeze kugombea nafasi mbalimbali pindi zikijitokeza ikiwemo uenyekiti wa vitongoji, vijiji, mitaa, udiwani na ubunge.


Massay alisema vijana wanapaswa kuchangamkia fursa hizo kwa kudhubutu kuchukua fomu na kuacha woga kwani hata yeye alianza kuwa chipukizi, UVCCM na hivi sasa ni mbunge. 

3 comments:

  1. So nice kijana hongera natamani kukuona nikirudi mkoani kwetu manyara by Rebeca Panga from babati magugu sarame karibu na huko kwetu jamani

    ReplyDelete
  2. So nice kijana hongera natamani kukuona nikirudi mkoani kwetu manyara by Rebeca Panga from babati magugu sarame karibu na huko kwetu jamani

    ReplyDelete
  3. So nice kijana hongera natamani kukuona nikirudi mkoani kwetu manyara by Rebeca Panga from babati magugu sarame karibu na huko kwetu jamani

    ReplyDelete