Saturday 11 June 2016

WAANDISHI WA MANYARA WAJENGEWA UWEZO KUANDIKA HABARI ZA INTANETI



Waandishi wa habari wa Mkoa wa Manyara, wamepatiwa mafunzo ya matumizi sahihi ya intaneti kwa uandishi wa habari wa kisasa kwa ajili ya kutafuta habari, mawasiliano ya mtandao, kuchapisha habari makazini mwao.
Kaimu mkurugenzi wa Taasisi ya vyombo vya habari kusini mwa bara la Afrika, tawi la Tanzania, Andrew Marawiti, akizungumza jana mjini Babati alisema mafunzo hayo yatawajengea uwezo wa matumizi sahihi ya intaneti.

Marawiti alisema mafunzo hayo yatawasaidia kutambua usalama wa teknolojia ya habari na umuhimu wake kwa waandishi, matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii, umuhimu wa kuzingatia maadili ya uandishi wa habari kwa intaneti.  
“Mafunzo hayo yamedhaminiwa na Misa Tan kwa kushirikiana na mfuko wa vyombo vya habari, mawasiliano na maendeleo Finland Vikes Foundation kwa msaada wa Wizara ya mambo ya nje ya Finland,” alisema Marawiti.



Kwa upande wake, mwezeshaji wa mafunzo hayo Seif Jigge alisema hayo ni mafunzo ya tatu kuyatoa kwa waandishi wa habari, kwani awali aliwaongezea uwezo wa habari za intaneti waandishi wa mikoa ya Mtwara na Kilimanjaro.

Jigge alisema kupitia mafunzo haya waandishi hao watakuwa na uwezo zaidi wa kupata taarifa zao kupitia vyanzo husika na kutambua namna ya kuhifadhi kwa usalama kwenye mafaili yaliyopo katika kompyuta ili zisivamiwe na virusi.



Mmoja kati ya mwandishi aliyeshiriki mafunzo Restituta Fissoo alisema alijifunza kupata habari kwenye vyanzo vya uhakika ikiwemo takwimu au habari za wizara kuliko kutafuta katika mitandao ya vyanzo visivyo na uhakika.

Mwandishi mwingine Baraka Ole Maika, alisema amejifunza mengi kupitia mafunzo hayo ikiwemo namna ya kuhifadhi taarifa zake kwa usalama zaidi, kufahamu teknolojia ya habari kwa upana wake na kupata anuani ya vyanzo vya habari.  

No comments:

Post a Comment