Saturday 11 June 2016

MAWAKALA WA PEMBEJEO MANYARA WATAKIWA KUWAJALI WAKULIMA


Katibu Tawala wa Mkoa wa Manyara, Eliakim Maswi amewataka mawakala wa pembejeo za kilimo wa mkoa huo, kuhakikisha wanazitoa huduma zao vyema kwa wakulima wa wilaya zote, ili waweze kujinyanyua kiuchumi.

Maswi alitoa agizo hilo mjini Babati, wakati akizungumza kwenye mapokezi ya vocha za ruzuku zilizobaki katika halmashauri za wilaya zilizopo katika mkoa huo kwa upande wa msimu wa kilimo wa mwaka 2015/2016.  

Aliwataka mawakala hao watoe taarifa kwake kwenye vikwazo vya kufanya biashara ya pembejeo za kilimo na endapo watendaji wa serikali watakuwa wanawataka wawape asante, wafikishe suala hilo ili wawachukulie hatua.

“Tunapaswa kutumia uzalendo jamani kwani hii nchi ni yetu na tutakaoijenga ni sisi wenyewe na pia tutakaoibomoa ni sisi sisi, hivyo tujipange kumsaidia mkulima wa kawaida katika kupata maendeleo ya kilimo,” alisema Maswi.

Alisema atawapa ushirikiano mawakala wote wa pembejeo ili kuhakikisha mkoa wa Manyara, unaendelea kupiga hatua katika suala zima la kilimo na wakulima wananufaika kupitia pembejeo watakazopatiwa msimu wa kilimo.

Hata hivyo, amewataka mawakala hao kuhakikisha wanatimiza wajibu wao ipasavyo kwani mkoa huo upo nyuma kimaendelea kwenye mambo mengi na kupitia kilimo wananchi wengi wataweza kupiga hatua kubwa tofauti na awali.

Kwa upande wake, ofisa kilimo wa mkoa wa huo, Coletha Shayo alisema halmashauri ya Babati mjini walibakiza vocha 1,157 za thamani ya sh34.865 milioni, Babati vijijini vocha 4,329 zenye thamani ya sh119.500 milioni.

Shayo alisema Hanang’ ilibakiza vocha 1,800 za sh54 milioni, Kiteto vocha 13,650 za sh407 milioni, Simanjiro vocha 5,943 za sh164.135 milioni, Mbulu vijini vocha 10,800 za sh225.645 milioni na Mbulu mjini vocha 7,589 za sh224 milioni.

No comments:

Post a Comment