Wednesday 8 June 2016

WAZIRI LUKUVI AZINDUA BARAZA LA ARDHI NA NYUMBA KITETO



Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya makazi, William Lukuvi amezindua Baraza la Ardhi na Nyumba la Wilaya ya Kiteto Mkoani Manyara, ambalo kwa kiasi kikubwa litamaliza migogoro ya ardhi iliyokuwa inawakabili wananchi wa eneo hilo.

Awali, wananchi wa wilaya hiyo iliwabidi wafuate huduma hiyo umbali wa kilometa 300 kwenda na kurudi wilayani Simanjiro ambapo kuna baraza kama hilo, ili kufungua mashauri yao kwenye masuala ya ardhi au nyumba.

Akizungumza wilayani Kiteto wakati akizindua baraza hilo, Lukuvi alisema baraza la Kiteto na Lushoto ni miongoni mwa mabaraza 47 yatakayozinduliwa hivi karibuni kwenye wilaya mbalimbali ambazo hazina mabaraza.



Alisema baraza hilo litawasaidia wananchi wa Kiteto kuondoa kero ya kufuata huduma hiyo wilayani Simanjiro kwani kati ya kesi 150 zinazofanyika kwa mwaka wilayani Simanjiro, kesi 100 zinawahusu watu wa wilaya ya Kiteto.

“Lengo la serikali ya awamu ya tano ya Rais John Magufuli ni kumaliza migogoro ya ardhi hivyo kupitia haya mabaraza ya ardhi na nyumba na katika vijiji tutaweka matumizi bora ya ardhi ili kusiwepo na migogoro,” alisema Waziri Lukuvi.

Alisema mpango wa matumizi bora ya ardhi utasababisha wakulima na wafugaji kutogombana kwani kila kijiji kitatenga eneo la mashamba, malisho ya mifugo, makazi, sehemu za ibada na huduma nyingine na kuondokana na migogoro.


Mkuu wa mkoa wa Manyara, Dk Joel Bendera alisema baraza hilo litasaidia kumaliza tatizo la migogoro ya ardhi iliyokithiri kwani awali wananchi wengi walikuwa wanafika mjini Babati kutoa malalamiko yao ya migogoro ya ardhi. 

Hata hivyo, Dk Bendera aliwataka Mwenyekiti wa baraza hilo la Kiteto Charles Mnzava na wazee wa baraza kutenda haki kwa wananchi wa Kiteto wakati wa kuendesha mashauri hayo ili jamii ione faida ya kuwepo kwa baraza hilo.

“Sasa wananchi waliokuwa wanakwenda Simanjiro kuhudumiwa wamerahisishiwa kwa kuletewa baraza hapa Kiteto ila isiwe njia ya kupokea rushwa na kuwa kero kwa jamii, tendeni haki ili watu waridhike,” alisema.

Mbunge wa jimbo la Kiteto, Emmanuel Papian alimshukuru Waziri Lukuvi kwa kuzindua baraza hilo kwani litasaidia kwa namna moja au nyingine kumaliza migogoro ya ardhi ambayo ilikuwa imekithiri kwenye eneo hilo la Kiteto.

“Kupitia baraza la ardhi na nyumba hapa Kiteto huu ndiyo utakuwa mwisho wa kuwepo kwa migogoro ya ardhi kwani awali tulikuwa tunateseka kwenda Simanjiro kwani jamii ilikuwa inatumia gharama kubwa,” alisema Papian.

Alitoa ombi kwa Waziri Lukuvi kusaidia upimaji wa viwanja vyote vya wilaya hiyo ili uwekwe kwenye mpango wa matumizi bora ya ardhi, kwani huo utakuwa mwisho wa migogoro yote ya ardhi iliyokuwa imekithiri Kiteto.

No comments:

Post a Comment