Saturday 7 February 2015

KWAYA YA MIRERANI CENTRAL SDA YAKABIDHI MSAADA WA MATOFALI 34



Shule ya msingi Endiamtu ya Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, yenye upungufu wa matundu 19 ya choo, imepatiwa msaada wa mifuko 34 ya saruji iliyotolewa na kwaya ya Mirerani Central ya Kanisa la Wasabato SDA. 

Katibu wa Kanisa hilo, Benson Nyaura akizungumza jana wakati akikabidhi mifuko hiyo 34 ya saruji kwa Diwani wa kata ya Endiamtu Lucas Zacharia alisema kanisa ni taasisi inayojali mahitaji ya jamii hivyo wamejitoa ili kusaidia wanafunzi hao.

Nyaura alisema kila wakati Kanisa hilo linashirikiana na wananchi katika kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazowakabili ili kuhakikisha kwa namna moja au nyingine wanatatua matatizo yanayoizunguka jamii.

Kwa upande wake, Diwani wa kata ya Endiamtu Lucas Zacharia aliwapongeza wana kwaya hao kwa kujitolea kiasi hicho cha saruji, ambapo ikichanganywa na fedha zilizotengwa, zitawezesha kujengwa kwa choo kingine cha shule hiyo.

Zacharia alisema alipochaguliwa kuwa Diwani mwaka 2010 alikuta shule hiyo ina majengo ya madarasa mawili na wanafunzi wa kuanzia darasa la kwanza hadi la sita, ila sasa wameongeza madarasa mengine manne na ofisi ya walimu.

“Mimi kwa kushirikiana na jamii na halmashauri ya wilaya ya Simanjiro, tumeweza kuiendeleza shule hii ambayo mwaka jana ifanya vizuri kwenye matokeo ya darasa la saba hivyo kuonga kitaaluma,” alisema Zacharia.



Naye, Ofisa mtendaji wa kata ya Endiamtu Edmund Tibiita alipongeza jitihada za Diwani huyo kuipa kipaumbele shule hiyo ya msingi ambayo awali ilikuwa inadharaulika kuwa ipo porini na sasa imepiga hatua kubwa hasa kitaaluma.

“Sasa hivi shule hii ina vyumba sita vya madarasa, kutoka vyumba viwili vilivyokuwepo mwaka 2010 na Diwani Lucas amechangia fedha zake binafsi sh5 milioni kwa ajili ya kuendeleza shule hii na anafaa kupongezwa,” alisema Tibiita.

No comments:

Post a Comment