Tuesday 8 May 2012


Na Joseph Lyimo

WAKAZI wawili wa Wilaya ya Babati Mkoani Manyara wameifikisha Mahakamani Halmashauri ya Mji wa Babati wakiitaka iwalipe fidia ya zaidi ya sh78 bilioni kwa madai ya kutaifisha maeneo yao bila kuwalipa fidia kwa muda wa miaka saba iliyopita

Wakazi hao wa mjini Babati Bruno Ngomuo na Idd Ngomuo wamefungua kesi hiyo jana Jumatatu katika Mahakama ya Ardhi Wilaya  ya Babati wakisimamiwa na wakili maarufu mkoani humo Westget Lumambo.


Kwa mujibu wa hati ya madai iliyofunguliwa Mahakamani hapo mjini Babati mbele ya Mwenyekiti wake Prosper Makundi walalamikaji hao wameitaka Mahakama hiyo iwahalalishie wamiliki hao maeneo hayo.

Imedaiwa kuwa kwa muda huo wote wamekuwa wakiahidiwa kulipwa fidia lakini hakuna utekelezaji wowote uliofanyika kwa takribani miaka saba.


Hati hiyo ilieleza kuwa tangu mwaka 2004 Halmashauri ya Mji wa Babati ilitaifisha maeneo ya jumla ya ekari nne na robo mali ya Bruno Ngomuo na Idd Ngomuo na kuyagawa maeneo hayo kwa watu wengine bila kuwalipa wao fidia ambayo ni haki yao ya msingi.

Walalamikaji hao wanadai kuwa kwa muda wote huo wamekuwa wakiahidiwa kulipwa fidia lakini hakuna utekelezaji wowote uliofanyika kwa takribani miaka saba hadi hivi sasa.


Hata hivyo kwa pande wa Halmashauri ya Mji wa Babati ambao ndiyo wadaiwa katika kesi hiyo wanasimamiwa na Mwanasheria wa halmashauri hiyo Reginald Mtei. 

Shauri hilo limeahirishwa hadi Juni 20 mwaka huu ambapo upande wa wadaiwa ambao ni Halmashauri ya mji wa Babati pamoja na wadai ambao ni Bruno Ngomuo na Idd Ngomuo wametakiwa kuleta utetezi wao.


MWISHO.

No comments:

Post a Comment