Thursday 13 October 2016

CRDB YAKABIDHI HOSPITALI YA HAYDOM MASHUKA 100

Benki ya CRDB imetoa msaada wa mashuka 100 kwenye hospitali ya rufaa ya Haydom Wilayani Mbulu Mkoani Manyara, kwa lengo la kuwasaidia wagonjwa wanaolazwa katika hospitali hiyo inayohudumia zaidi ya watu wa mikoa minne nchini.

Akizungumza wakati akikabidhi mashuka hayo 100 kwa mkurugenzi wa hospitali hiyo Dk Emanuel Nuwass, Meneja wa CRDB Tawi la Babati Ronald Paul alisema wanatoa msaada huo ili kurudisha hisani kwa jamii.

Paul alisema wamekabidhi mashuka hayo ili kutoa asante kwa jamii kwenye wiki ya huduma kwa wateja, kwa kurudisha kwao kile kidogo wanachopata kwa ajili ya kuboresha mahusiano zaidi baina ya benki hiyo na wateja wake.

“Tutaendelea kushirikiana na kusaidiana kwenye masuala mbalimbali ya kijamii kwani tunatambua jitihada na changamoto ya hospitali ya Haydom ambayo inatoa huduma kwa watu wa Manyara na waliopo mikoa ya jirani,” alisema.

Hata hivyo, mkurugenzi wa hospitali hiyo Dk Emanuel Nuwass alisema hii ni mara ya tatu kwa benki hiyo kutoa msaada kwenye hospitali ya Haydom, hivyo iendelee kuwa karibu nao kwa ajili ya kupeana ushirikiano wa kusaidia jamii.

Dk Nuwass alisema awali benki hiyo ilitoa mchango wa maendeleo wa sh1 milioni kwa ajili ya siku ya Haydom, kisha wakawapa zawadi ya ng’ombe mmoja mkubwa wa siku ya familia na mashuka 100 yatakayotumiwa na wagonjwa.

Alisema hivi karibuni bodi ya hospitali hiyo ilikubaliana na mpango wa malipo kwa wagonjwa kupitia njia ya kadi ya CRDB na zoezi hilo linatarajia kuwarahisishia watu wote watakaopata huduma katika eneo hilo la Haydom.

Kwa upande wake, meneja masoko mwandamizi wa benki hiyo Fredrick Siwale alisema benki hiyo itandelea kutoa huduma nzuri kwa wateja wao huku ikiboresha maeneo ambayo huduma haipatikani kwa kuhakikisha wanakuwepo.

“Kupitia kauli mbiu yetu ya ulipo tupo kama hatupo tutakuja na kama hatujaja utusubiri, tunalenga kuwahudumia watanzania wote na kupitia hilo ndiyo sababu tukafika kutoa mashuka haya kwani tunaithamini jamii,” alisema Siwale.

No comments:

Post a Comment