Wednesday 21 September 2016

WALIA NA HUDUMA MBOVU KITUO CHA AFYA MIRERANI


Wagonjwa wanaopata huduma kituo cha afya Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, wameiomba Serikali kuchukua hatua na kuboresha matibabu kwenye kituo hicho kwani hivi sasa huduma nyingi zimedorora.

Wakizungumza kuhusu changamoto hiyo wagonjwa hao walidai kuwa huduma zinazotolewa hivi sasa kwenye kituo hicho ni vipimo, kliniki ya mama na mtoto na vidonge vya kufubaza virusi vya ukimwi (ARV) pekee.

Mmoja kati ya wagonjwa hao John Benarld alisema hivi sasa kituo hicho kina hali mbaya mno kwani hata dawa zimekuwa tatizo, hadi kusababisha wagonjwa kudhani kuwa wauguzi wanauza dawa kwenye maduka yao kumbe sivyo.

“Tunaiomba serikali iingilie kati suala hili kwani ni aibu hata maji ya drip hawana, dawa hakuna hata paracetamol hazipo na pia hivi sasa ni zaidi ya miezi mitatu maji ya bomba yamekatika katika kituo hicho cha afya,” alisema Bernald.

Selemani Mohamed alisema hata upungufu wa watumishi ni tatizo kwani alitumia muda wa saa mbili kukaa kwenye kiti kwa ajili ya kupata huduma ya vipimo kwenye maabara kutokana na kuwepo na mtumishi mmoja pekee.

“Nimetoka kwa daktari muda mrefu na mtoto wangu mdogo anaumwa nimeambiwa niende eneo la maabara akachukuliwe kipimo cha damu lakini bado sijapatiwa huduma huyu dada yupo peke yake,” alisema Mohamed.

Alisema kitengo cha maabara kinapaswa kiwe na wahudumu wawili au watatu kwani kuna wagonjwa wengine wanafika kituoni hapo wakiwa wana hali mbaya ya kuzidiwa ila hivi sasa kuna mtaalamu mmoja anayehudumia watu wengi.
Hata hivyo, mganga mfawidhi wa kituo hicho Dk Raymond Msaki alikiri kuwepo na upungufu wa dawa kwani wagonjwa wengi wamekuwa wanakosa huduma kutokana na upungufu huo, ila uongozi ulishafikisha taarifa sehemu husika.

Dk Msaki pia alikiri kuwepo na tatizo la maji kwenye kituo hicho kwani tangu mwezi Julai maji yaliyounganishwa na mamlaka ya mji mdogo hayapatikani ila wakitaka maji wanaomba kwa jirani yao kulikokuwa na shirika la World vision.

“Upungufu wa watumishi ni kweli kwani sehemu ya maabara hivi sasa kuna dada mmoja yeye ndiye anaandika wagonjwa anawapima na kutoa majibu, wenzake wawili hawapo, mmoja yupo masomoni na mwingine yupo likizo,” alisema.

No comments:

Post a Comment