Thursday 4 February 2016

WATAKA KAMPUNI YA TANZANITEONE IONDOLEWE



Wachimbaji wa kampuni ya TanzaniteOne ya Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, wameiomba Serikali iiondoe kampuni hiyo kwani imeshindwa kujiendesha hadi kushindwa kuwapa chakula na maji.

Wakizungumza juzi mbele ya kamati ya ulinzi na usalama ya mikoa ya kanda ya kaskazini, wachimbaji hao walidai kuwa hivi sasa wanafanya kazi kwenye mazingira magumu kutokana na uwezo mdogo wa kampuni hiyo kujiendesha.

Mmoja kati ya wafanyakazi hao Sophia Mbimbi alisema wamekuwa na wakati mgumu wa kufanya kazi kwani kila siku wanakula chakula cha aina moja na hata maji ya kunywa inabidi mfanyakazi ajinunulie dukani ili ashuke nayo mgodini.

“Kampuni inayochimba mgodi mkubwa wa Tanzanite kuliko yote duniani inashindwa kuwa na hata maji safi na salama na kununua maji yanayotoka wilayani Hai, huko ni kutusononesha na kutushangaza sana,” alisema Mbimbi.




Mchimbaji mwingine Aven Mwaitalako alisema kampuni hiyo imeshindwa kufanya kazi kwani tangu wanunue hisa imekuwa inaendesha mambo yake bila kuwa makini hadi kufikia hatua ya kupiga nguzo badala ya kubuni eneo.

“Imefikia hatua ya kufuata nguzo zilizoachwa na mzungu zilizokuwa zinatoa madini na ndizo tunapiga baruti, badala ya kutafuta njia zetu nyingine ili tuoe madini, kweli kampuni hii imejichokea,” alisema Mwaitalako.

Kwa upande wake, Raphael Ombade alisema suala la wafanyakazi kupekuliwa kwa kuvuliwa nguo siyo zuri kwani  ni udhalilishaji wa utu wa mtu na pia mionzi iliiyokuwa inawapekua awali ilikuwa ya mizigo hivyo isirudishwe tena.




Hata hivyo, meneja wa mgodi huo, Modest Apolinary alisema uongozi wa kampuni hiyo umejipanga kurekebisha mapungufu yaliyojitokeza na kila wakati watakuwa wanakutana na uongozi wa wachimbaji ili kujadili kwa pamoja.

“Pamoja na hayo sisi ni watanzania jamani kwani mlitaka kula chakula gani na haya maji mtaalamu wetu ametuhakikishia ni masafi na salama kwani yametoka hapo Boma Ngombe wilayani Hai, hayana tatizo,” alisema.

Akizungumza na uongozi na wafanyakazi wa kampuni hiyo, Mwenyekiti wa kamati hiyo ambaye ni mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro, Amosi Makala alisema ameiagiza TanzaniteOne iwekeze fedha nyingi zaidi ili ipate madini zaidi.

“Mtakuwa mnafanya ubabaishaji sasa, hadi mnapiga nguzo za zamani jamani, wekezeni mtaji mkubwa ili mpate madini na siyo kuwa kama mnavuna majani na kuokota karanga zilizobakia shambani,” alisema Makala.

No comments:

Post a Comment