Sunday 31 January 2016

KITETO WACHANGAMKIA KUJIUNGA NA CHF



Wakazi wa Wilaya ya Kiteto, Mkoani Manyara, wametakiwa kujiunga na mfuko wa afya ya jamii (CHF) ili waweze kupatiwa matibabu kwa kuchangia sh10,000 na kupatiwa matibabu mwaka mzima kwa kaya yenye watu sita.

Akizungumza kwenye kijiji cha Engusero wakati wa uzinduzi wa uhamasishaji wa kaya kujiunga na CHF, mkuu wa wilaya hiyo Kanali Samuel Nzoka alisema kaya nyingi zikijiunga ndiyo upatikanaji wa dawa unakuwepo.

Kanali Nzoka alisema tatizo la ukosefu wa dawa kwenye zahanati, vituo vya afya na hospitalini litamalizika, endapo kaya nyingi zikijiunga na CHF kwani serikali nayo itaweka mkono wake ili kuhakikisha huduma za afya zinaboreshwa.

Wakati wa uzinduzi wa zoezi hilo Kanali Nzoka alijitolea sh20,000 kwa ajili ya kuzilipia kaya mbili za watu 12 wa kijiji cha Engusero na Dosidosi na kuungwa mkono na viongozi wanne wa wilaya hiyo waliojitolea sh10,000 kwa kila mmoja.




Meneja wa mfuko wa Taifa wa Bima ya afya (NHIF) wa mkoa wa Manyara, Isaya Shekifu alisema mwanachama wa CHF atanufaika na huduma zote za afya za msingi na kinga na tiba kwa zahanati, kituo cha afya na hospitali.




Shekifu alitaja baadhi ya huduma zinazotolewa ni vipimo vya maabara, wagonjwa wa kutwa na kulazwa, upasuaji kulingana na utaratibu uliowekwa na halmashauri husika na wanachama kupata huduma  bora ya afya kwa mwaka.

“Pia watapata huduma ya upasuaji kulingana na utaratibu uliowekwa na Halmashauri zinazoendesha mifuko hii zinapata mapato ya tele kwa tele kutoka serikalini ambayo yatatumika kuboresha huduma za afya,” alisema.

No comments:

Post a Comment